Pages

Wednesday, July 4, 2012

Mashekhe wataka Waislamu nchini kutopuuzia sensa

TAASISI ya Mashekhe na Wanazuoni wa Kiislamu nchini, imeunga mkono kauli ya hivi karibuni ya Shekhe Mkuu wa Tanzania, Mufti Issa Shaaban Simba ya kuwataka Waislamu na Watanzania kote nchini kushiriki kikamilifu katika Sensa ya Watu na Makazi itakayofanyika Agosti 26 mwaka huu.

Akizungumza jana kwa niaba ya Mwenyekiti wa Jopo la Mashekhe na Wanazuoni wa Kiislamu nchini, mmoja wa mashekhe hao, Shekhe Hamis Mattaka alisema wamelazimika kufanya hivyo kutokana na kuwepo kwa baadhi ya makundi yanayowapotosha waumini wa dini ya Kiislamu na wananchi juu ya ushiriki wao katika sensa.

Alisema wao kama jopo la wanazuoni, hawaoni tatizo la zoezi hilo kutokana na umuhimu wake kwa taifa na kuongeza kuwa Sensa ya Watu na Makazi ipo kwa mujibu wa sheria za nchi na imepitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Jopo hilo limeiomba Serikali kuweka sheria itakayozuia utoaji wa takwimu zinazohusu dini za Watanzania zinazotolewa na vyanzo mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa kuwa kipengele hicho si sehemu ya sensa nchini.

“Tunajua kuwa Serikali ilikuwa na nia njema kukiondoa kipengele cha dini katika sensa hapana budi nia njema hiyo ya Serikali ilindwe kwa kuweka sheria itakayozuia kutoa takwimu zinazohusu dini za Watanzania” amesema Shekhe Mattaka.

Alifafanua kuwa, sensa ya awali ya mwaka 1957 kipengele cha dini kilihusishwa na baadaye kuondolewa katika sensa zilizofuata kwenye madodoso ya kukusanyia takwimu za kaya.

“Sisi kama jopo kila siku tunasema ili twende salama kama wananchi wa nchi hii ni wajibu wetu kuheshimu na kufuata sheria kwa maana ya kutii sheria bila shuruti, kwa hiyo tunasema Sensa ya Watu na Makazi ni jambo la kisheria si jambo la mitaani, hatuwezi kulumbana na kujadili jambo ambalo liko wazi kisheria na limepitishwa na wabunge tuliowachagua sisi wenyewe.”

Aliongeza kuwa, Sensa ya Watu na Makazi itaiwezesha Serikali kupanga mipango ya maendeleo kwa kuwa na takwimu sahihi za watu na makazi, hali ya kipato cha kaya, vizazi na vifo na pia kuiwezesha Serikali kuwapatia huduma bora wananchi wake.

Katika hatua nyingine jopo la mashekhe na wanazuoni wa Kiislamu Tanzania imewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika mchakato wa ukusanyaji wa maoni ya Katiba mpya.

via HabariLeo

No comments:

Post a Comment