Pages

Monday, October 21, 2013

UNYAMA WA KUTISHA MGODI WA GEITA,UMEKUWA SEHEMU YA MAUAJI‏.

MGODI wa dhahabu wa Geita(GGM)uliopo mjini Geita,Umegeuka shubiri kwa baadhi ya wakazi wa wilaya hiyo na wilaya jirani kufuatia walinzi wake kugeuka kuwa wakatili wakubwa wa kushambulia watu na kusababisha vifo vyao.

Hali hiyo imesababisha matukio ya watu kufa wakiwa ndani ya mgodi huo kuzidi kuongezeka kila mara baada ya mtu mwingine,Zacharia Tabaro(36)mkazi wa mtaa wa Ibisabageni mjini Sengerema mkoani Mwanza kudaiwa kufa kwa kushambuliwa na walinzi wa mgodi huo.

Mwili wa marehemu Zacharia Tabaro(36)anayedaiwa kuuawa ndani ya mgodi wa Geita.
Shughuli za Mazishi ya marehemu Zacharia Tabaro(36)yaliyofanyika katika makaburi ya Sengerema Mision.
Mwanaume huyo inasemekana alishambuliwa na walinzi kwa vitu vyenye ncha kali pamoja na mawe na kusababisha kufariki dunia.

Tukio hilo limetokea usiku wa octoba 16,mwaka huu ambapo inadaiwa marehemu aliingia mgodini humo kwa muda usiojulikana kwenda kuchukua mawe yanayosadikika kuwa na dhahabu maarufu kwa jina la Magwangala.

Mmoja wa ndugu wa marehemu, Mengi Paulo alisema Tabaro aliondoka Mugusu mjini Geita jumapili ya wiuli iliyopita katika mazingira ya kutatanisha na juhudi za kumtafuta zilifanyika bila mafanikio ya kumpata.

Alisema hadi siku ya octoba 16 majira ya alfajiri walipopata taarifa kwa njia ya simu kutoka kwa baadhi ya wafanyakazi wa mgodi huo kwamba kuna mtu amekufa ndani ya mgodi.
Alisema baada ya taarifa hizo saa 3 asubuhi waliingia mgodini humo na kuikuta maiti ya ndugu yao ikiwa na jeraha kubwa lililotoboa paji la usoni linalotokana na kupigwa kwa mawe huku kifuani akiwa amewekewa jiwe zito.

Alipoulizwa kama ndugu yao ameuawa na walinzi wa mgodi huo,Paulo alisema inawezekana kutokana na kwamba walinzi wanapowaona watu mgodini humo wakiwa wameingia bila taratibu huwapiga,kwa mawe na wengine huwatumbukiza ndani ya mashimo marefu.
"Matukioya watu kupigwa,hili sio la kwanza mara nyingi yanajitokeza,watu wengi wamepoteza maisha ndani ya mgodi huo"alisema Paulo ambaye ni mpwa wa marehemu.

Ofisa habari wa Mgodi wa Geita(GGM),Tenga Birri Tenga,alipotafutwa kwa njia ya simu kuzungumza kama walinzi wa mgodi huo wamehusika katika  mauaji ya mtu huyo alisema taarifa hizo sio za kweli.
"Sio kweli ndugu yangu,huyo mtu hajauawa na walinzi,isipokuwa wao wenyewe wachimbaji wadogo walimpiga na baada ya kumuua walichukua mwili wake na kuutupa mgodini"
Hata hivyo alipouliza anathitishaje kuhusiana na kauli yake alisema sio mara ya kwanza mara nyingi wao wachimbaji wanapotoautiana katika kazi zao hushambuliana na kuuana.
Kaimu kamanda wa polisi mkoani Geita,Pundensiana Protas alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo kwa njia ya simu baada ya kuwa nje ya ofisi,simu yake ilipokelewa na mlinzi wake ambaye alidai kwamba alikuwa kwenye kikao.
Hata hivyo mwili wa marehemu ulichukulia na polisi kutoka mgodini humo na kupelekwa katika hospitali ya wilaya ya Geita,kwa uchunguzi zaidi ingawa majibu ya uchungizi hayakubainisha chanzo cha kifo hicho.
Daktari aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu bila kutaja jina lake kwa kuwa sio msemaji wa hospitali hiyo,alisema majibu yatatolewa hapo baadaye na uongozi husika.
Takwimu zinaonyesha kuwa watu zaidi ya 30 wamekufa ndani ya mgodi huo katika kipindi cha kuanzia januari mwaka jana hadi septemba mwaka huu.
Mwisho.

Habari na Salum Maige,Geita.

No comments:

Post a Comment