Pages

Sunday, December 1, 2013

Wanafunzi: Uamuzi Kamati Kuu Chadema sawasawa

Dar es Salaam.  
Shirikisho la Wanafunzi wa Elimu ya Juu Mkoa wa Dar es Salaam wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), CHASO limekanusha habari kuwa wanapinga uamuzi wa Kamati Kuu ya chama chao kuwavua uongozi baadhi ya wanachama wao.

Kamati Kuu ya Chadema hivi karibuni kiliwavua uongozi Zitto Kabwe, Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba kwa tuhuma za hujuma dhidi ya chama na kwenda kinyume na katiba.
Himida Elihuruma, Mratibu Mkuu wa CHASO Dar es Salaam, alisema siyo kweli wanahusika kupinga uamuzi wa kamati kuu na kwamba waliosambaza taarifa hizo hawana nia nzuri.

“Hao waliotoa taarifa hizo ni wanafunzi feki wa vyuo vikuu. Ni propaganda za Chama Cha Mapinduzi (CCM), hawajazowea kufanya uamuzi mgumu kwa maslahi ya nchi,” alisema Elihuruma.
“Tunapenda kuliweka wazi suala hili kwamba, tunaungana na uamuzi uliofikiwa wa kuwavua uongozi viongozi wanaotuhumiwa kutaka kukihujumu chama,” alisema.
Elihuruma anasema aliyeandaa mkutano huo ni Mtela Mwampamba, ambaye walishamvua uongozi, hivyo inaonyesha ni kwa kiasi gani watoa habari hawakuwa sahihi.

Naye Julius Maiko ambaye ni Mwenyekiti wa CHAKO Mkoa wa Dar es Salaam, alisema kuwa CCM ni watetezi wa maovu kwani wameshindwa kuchukua uamuzi mgumu kuwawajibisha viongozi wazembe.

Akitoa mfano, Julius alisema Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana anazunguka nchi nzima na miongoni mwa hotuba zake, anawataja viongozi mizigo lakini, wanashindwa kwa kuwa hawajazoea kufanya uamuzi mgumu kama wa Chadema.
Elihuruma alisema: “Msimamo wa CHASO unaunga mkono uamuzi wa kamati kuu ya kuwavua uongozi baadhi ya wanachama. Tunataka kuona chama kinakuwa na viongozi wazuri.”CREDIT: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment