Pages

Saturday, December 29, 2012

John Mnyika, Zitto, wabunge bora 2012

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), kwa sasa ndiye anashikilia rekodi ya ukinara wa kuchangia mara nyingi bungeni kwa mwaka 2012, akifuatiwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA) na Godfrey Zambi wa Mbozi Mashariki (CCM).

Kwa mujibu ya rekodi zalizomo kwenye mtandao wa Bunge, Mnyika ambaye ni kipindi chake cha kwanza bungeni, ameonekana kufanya vizuri zaidi sambamba na wabunge wenzake kadhaa wa CHADEMA.
Takwimu hizo hazijawahusisha mawaziri, manaibu wao, Spika, naibu wake, wenyeviti watatu wa Bunge, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa vile nafasi zao zinawapa uwezekano mkubwa wa kuchangia hoja wakati wowote.

Wabunge kumi ambao wameshika nafasi za juu ni Mnyika akiwa amechangia mara 184, kuuliza maswali ya nyongeza 28 na ya msingi 7, akifuatiwa na Zitto (mchango 79, maswali ya nyongeza 25 na maswali ya msingi 8) wakati Zambi anashika nafasi ya tatu kwa kuchangia mara 70, (maswali nyongeza 26) na (maswali ya msingi 9).

Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu anashika nafasi ya nne akiwa amechangia mara 93, maswali ya nyongeza 19 na yale ya msingi 7, akifuatiwa na Diana Chilolo wa Viti Maalumu (CCM) aliyechangia mara 61, maswali ya nyongeza 41 na msingi 9.

Nafasi ya sita inashikiliwa na Halima Mdee wa Kawe (CHADEMA) akiwa na rekodi ya michango 59, maswali ya nyongeza 15 na ya msingi 6 akifuatiwa na Moses Machali wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi) mwenye michango 57, nyongeza 30 na maswali ya msingi 7.
Magdalena Sakaya wa Viti Maalumu (CUF) ameshika nafasi ya nane akiwa na michango 52, maswali ya nyongeza 13 na ya msingi 4, huku Mbunge wa Kisarawe, Seleman Jafo (CCM) akifuatia kwa michango 51, maswali nyongeza 10 na ya msingi 6.

Anayefunga dimba kwa kumi bora ni Ester Bulaya wa Viti Maalumu (CCM) mwenye michango 47, maswali ya nyongeza 17 na maswali ya msingi 3, akiwa amefungana na Martha Mlata wa Viti Maalumu (CCM) mwenye rekodi ya michango 47, maswali ya nyongeza 11 na ya msingi 5.
Ni takriban miaka miwili tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu, ambapo vyama vya upinzani hususan CHADEMA, wabunge wake wameendelea kuonesha umahiri bungeni.
Hata Bunge la tisa lililopita kwa mujibu wa utafiti wa shirika moja, Zitto na Dk. Willibrod Slaa akiwa mbunge wa Karatu wakati huo, walishika nafasi za juu.
Katika mtiririko huo wa takwimu hizo kwenye mtandao wa Bunge, wabunge wanaoonekana kuwa na alama ndogo wengi ni wale wa Viti Maalumu CCM na baadhi wa CUF.

No comments:

Post a Comment