Pages

Friday, March 29, 2013

Watanzania 235 wakamatwa na ‘unga’

WATANZANIA 235 wanaojihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya nje ya nchi wamekamatwa.

Kamishna wa Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya Nchini, Christopher Shekiondo, alibainisha hayo jijini Dar es Salaam jana alipozungumza na waandishi wa habari.
Shekiondo alisema Watanzania hao wamekamatwa kuanzia mwaka 2008 hadi mwaka jana katika nchi za Brazil, Kenya, China, Pakistan, Falme za Kiarabu na Mauritius.

Kwa mujibu wa kamishna huyo, baadhi ya Watanzania wamehukumiwa adhabu ya kifungo cha maisha na wengine adhabu ya kifo.
Aidha alisema jumla ya kilo 728.3 za heroin zilikamatwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2008 hadi 2012 na kwamba kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu kilo 12 za dawa hizo zilikamatwa.

“Pia kilo 352.3 za cocaine zilikamatwa kati ya 2008 hadi 2012, kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu kilo tatu za cocaine zilikamatwa,” alisema.
Aliongeza katika kipindi hicho watuhumiwa 149 walikamatwa na kufikishwa mahakamani kati ya mwaka 2010 na 2012 kwa makosa mbalimbali ya kujihusisha na biashara hiyo.
Kwa mujibu wa kamishna huyo, kati ya mwaka 2010 hadi 2012, kilo 96.88 za heroin ziliteketezwa katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Mtwara na Lindi.

No comments:

Post a Comment