Pages

Saturday, September 28, 2013

Watatu EPA waenda jela

Habari na Happiness Katabazi wa Tanzania Daima.
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imewahukumu kwenda jela miaka tofauti washitakiwa watatu waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya wizi wa sh bilioni 1.1 katika akaunti ya madeni ya nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania.

Hatua hiyo ni baada ya kuwakuta na hatia katika makosa mbalimbali, likiwemo la kughushi hati ya kuhamisha deni toka Kampuni ya Marubeni ya Japan kwenda Kampuni ya Changanyikeni Residential Complex ya nchini.

Hukumu hiyo ya kesi ya jinai iliyokuwa ikiwakabili Bahati Mahenge, Manase Makalle, Davis Kamungu, Geofrey Mosha na Edda Mwakale ambaye ni mke wa mshitakiwa wa pili, ilitolewa na jopo lililokuwa likiongozwa na Jaji Sekela Mushi, Jaji Sam Rumanyika na 

Hakimu Mkazi Lameck Mlacha ambaye aliisoma kwa niaba ya wenzake.
Mlacha alisoma hukumu hiyo kwa kuanza kuikumbusha mahakama kuwa hati ya mashitaka ilikuwa na mashitaka tisa na kwamba kosa la kwanza ni kula njama kinyume na kifungu cha 384 cha sheria ya kanuni ya adhabu ya mwaka 2002.

Alisema kuwa washitakiwa hao walitenda kosa hilo kati ya Desemba 23 mwaka 2003 na Oktoba 26 mwaka 2005, ambapo kwa pamoja na watu wengine ambao hawapo mahakamani walitenda kosa hilo na kuiibia BoT.

Hakimu Mlacha alisema baada ya kupitia ushahidi na vielelezo vyote, mahakama yake inawatia hatiani Mahenge na Manase na kuwahukumu kwenda jela miaka mitano huku akiwaachia huru washitakiwa wengine.

Katika kosa la pili la kuwasilisha nyaraka za kutaka kampuni yao ya Changanyikeni isajiliwe na Brela huku wakionyesha jina la kufikirika la Samson Mapunda kuwa ndiye mkurugenzi wa kampuni hiyo, hakimu Mlacha pia alisema Mahenge na Manase walitenda kosa hilo na hivyo mahakama yake inawahukumu kwenda jela miaka mitano.

Kosa la tatu lilikuwa likimkabili Mahenge pekee akidaiwa kutoa nyaraka za uongo za kuomba usajili wa kampuni zikionyesha Mapunda ndiye mkurugenzi wa Changanyikeni, na hivyo kuwezesha kampuni hiyo kupewa usajili na Brela. Mahakama ilimtia hatiani na kumfunga miaka saba gerezani.

Hakimu Mlacha alilitaja kosa la nne kuwa la Kampuni ya Changanyikeni Residential Complex, ambalo washitakiwa wamejipatia usajili toka Brela kwa nia ya udanganyifu kwa kutumia jina la kufikirika ambapo mahakama iliwatia hatiani tena Mahenge na Manase kwa kuwahukumu kifungo cha mwaka mmoja jela.

Katika kosa la tano la kughushi ambalo linawakabili washitakiwa wote, hakimu alisema katika maelezo ya onyo alilowapa wachunguzi wa kesi hiyo, Mahenge alikiri kuwa yeye alikuwa akitumwa kuchukua hundi za malipo ya kampuni hizo mbali na kwamba ndiye aliyekwenda kupeleka fomu Brela za kusajili kampuni yao ya Changanyikeni.

Alisema kuwa Mahenge alikuwa akisaidiana kufanya kazi hiyo na mshitakiwa Manase, hivyo mahakama hiyo imewatia hatiani Mahenge na Manase na Edda ambao ni mke na mume na kwamba watakwenda jela miezi 18.

Kosa la sita liliwakabili washitakiwa wote ambalo ni la kughushi hati ya kuhamisha deni lililokuwa likionyesha Kampuni ya Marubeni ya Japan imeridhia Kampuni ya Changanyikeni idai deni lake jambo ambalo si kweli.

“Licha upande wa utetezi kudai hati hiyo ya kuhamisha deni ilikuwa ni halisi, lakini sisi kama mahakama tulipata wasaa tukaikagua kwa makini, tukabaini hata hiyo kampuni ya Marubeni haikutia saini katika hati hiyo, na kampuni ya Changanyikeni ilisaini hati hiyo bila kuwepo shahidi wa kushuhudia tukio hilo.

“Hati hiyo inaonyesha ilisainiwa katika mgahawa wa City Garden Dar es Salaam, na tulijiuliza Marubeni ni kampuni kubwa kwanini haikutia saini katika hati hiyo, na mwisho wake mahakama hii ikakubaliana na upande wa jamhuri kuwa hati hiyo ilikuwa imeghushiwa,” alisema.

Alisema kuwa kwa kosa hilo, mahakama inawatia hatiani Mahenge na Manase na hivyo wataenda jela miezi 18.

Shitaka la saba liliwakabili washitakiwa wote ambalo ni la kuwasilisha hati hiyo ya kuhamisha deni iliyoghushiwa na kwamba mahakama yake imemtia hatiani Mahenge ambaye atakwenda jela mwaka mmoja.

Kuhusu shitaka la nane ambalo ni wizi na shitaka la tisa lilikuwa ni la kujipatia kiasi hicho cha fedha toka BoT, hakimu Mlacha alisema mahakama yake inawaachilia huru katika makosa hayo mawili.

Hata hivyo hakimu Mlacha alisema ushahidi ulioletwa na upande wa jamhuri umeshindwa kuishawishi mahakama imuone mshitakiwa wa tatu (Davis Kamungu) na wanne (Geofrey Mosha) wana hatia katika kesi hiyo na kwa sababu hiyo ikawaachilia huru.

Baada ya hakimu Mlacha kuwatia hatiani washitakiwa hao, wakili Mwanadamizi wa serikali Shadrack Kimaro alidai upande wa jamhuri hauna rekodi za uhalifu za washitakiwa waliotiwa hatiani ila wanaiomba itoe adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine.

Aliomba mahakama itumie kifungu 384(1) na 358(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, kuwaamuru washitakiwa waliotiwa hatiani kurejesha kiasi hicho cha fedha serikalini.

Kwa upande wake wakili wa washitakiwa, Tarimo, aliomba mahakama iwapatie adhabu ndogo kwani hii ni mara yao ya kwanza kukutwa na hatia, na kwamba Manase na Edda ni mke na mume wana familia inawategemea na kudai kuwa Edda anasumbuliwa na maradhi ya uzazi hivyo anaomba wapewe adhabu ndogo.

Hakimu Mlacha alisema amesikiliza maombi ya pande zote mbili na kwamba mahakama hiyo inaamuru Mahenge na Manase warejeshe kiasi hicho cha fedha na kwamba adhabu hiyo itakwenda pamoja.

Kwa maana hiyo Mahenge peke yake atakwenda jela miaka saba, Manase mitano na Edda miezi 18.

Baada ya hukumu hiyo kumalizika kusomwa baadhi ya ndugu na jamaa wa washitakiwa hao waliangusha vilio mahakamani hapo na wanausalama waliwachukua wafungwa hao na kuwapeleka gerezani.

Novemba 2008, Wakili Kiongozi wa Serikali Stanslaus Boniface ambaye sasa ni marehemu alidai washitakiwa hao walitenda makosa hayo.
Hii ni kesi ya tano sasa ya EPA kati ya kesi 12 zilizofunguliwa mahakamani hapo Novemba 2008 na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk. Eliezer Feleshi kufuatia kumalizika kwa uchunguzi wa Tume ya Rais Jakaya Kikwete ya kuchunguza wizi huo.

No comments:

Post a Comment