WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Terezya
Huvisa, amesema ametishiwa kuuawa endapo ataendelea na zoezi la kubomoa
nyumba za watu zilizo kwenye maeneo oevu.
Madai hayo aliyatoa jana mjini hapa, alipokuwa akizungumza na
waandishi wa habari ambapo alisema amepigiwa simu za vitisho hivyo kwa
lengo la kukwamisha jitihada zake za kuwashughulikia wanaovunja sheria.
Alisema baada ya kupata vitisho hivyo, aliamua kuwapigia simu lakini
simu hizo hazikupatikana jambo lililomfanya kuvipuuzia vitisho hivyo.
“Sijaviripoti polisi vitisho, najua lengo lao lilikuwa kunitisha ili
nisiendelee na mkakati wa kuwabomolea nyumba wale waliojenga kwa kukiuka
sheria, wanajidanganya nitaendelea kuwabomolea,” alisema.
Alisema mtu yeyote mwenye jambo lenye tija na masilahi kwa taifa kamwe
asingesita kumpigia simu na ikiwezekana kwenda kumuona juu ya
bomoabomoa lakini waliompa vitisho hivyo ni ‘feki’.
Waziri huyo aliongeza kuwa Mwanasheria la Baraza la Taifa la Hifadhi
ya Mazingira (NEMC), Heche Manchare, naye alipewa vitisho pamoja na
kupigwa na watu waliokuwa wamevalia vitambaa usoni kwa lengo la kuficha
sura zao.
Alibainisha kuwa tukio hilo waliripoti kwa Makamu wa Rais, Dk. Mohamed
Gharib Bilal, ambaye aliwaambia walifikishe polisi lifanyiwe uchunguzi
zaidi.
Aliongeza kuwa pamoja na vitisho hivyo kamwe wizara yake haitarudi
nyuma katika zoezi la kuwabomolea nyumba, hoteli au wawekezaji wowote
wale waliojenga kwenye maeneo oevu.
“Hili ni zoezi gumu sana linalohitaji ujasiri na umakini mkubwa sana,
sisi hatutamuonea mtu yeyote, tumedhamiria kufanya kazi zetu kwa nguvu
hatarudi nyuma,” alisema.
Wiki iliyopita Waziri wa Mambo ya Ndani, Emanuel Nchimbi, aliwataka
viongozi na wananchi wote wanaopata vitisho kuwasiliana na polisi ili
hatua zichukuliwe.
Katika hatua nyingine, serikali imeeleza kupata hasara ya sh bilioni
50 kwenye utekelezaji wa zoezi la bomoabomoa katika fukwe za kawe na
mbezi jijini Dar es Salaam.
Waziri Huvisa, alisema kuwa kiasi hicho cha fedha ambacho serikali
imekitumia ni kikubwa sana na kitalipwa na wamiliki wa nyumba hizo ambao
walijenga kinyume cha sheria na watazigawanya kwa viwango mbalimbali
kutokana na kila nyumba ilipokuwa imefikia.
Alisema kuwa wizaya yake ilishirikiana na Maliasili na Utalii, Wizara
ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Manispaa ya Kinondoni ambapo
jumla ya nyumba saba na uzio nane zilibomolewa na ujenzi uliokuwa
unaendelea kwenye mkondo wa mto umebomolewa.
Alisema kuwa ubomoaji huu ni utekelezaji wa sheria ya mwaka 2004
kutokana na wananchi hao kukaidi na kutokutekelezwa kwa maagizo
mbalimbali ya kutoendelea na ujenzi yaliyotolewa kwa wahusika.
“Nawataka wale wote waliojenga na wanaoendelea kujenga kwenye vyanzo
vya maji, kando kando ya bahari, maziwa, mito na mabwawa na misitu
inayolindwa kisheria kuondoka mara moja na endapo watakiuka maagizo hayo
hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao,” alisema waziri huyo.
Alifafanua kuwa hatua zitakazochukuliwa dhidi yao moja wapo ni
kuwabomolea nyumba zao na kuwaondoa katika maeneo hayo na kwamba
watatakiwa kulipia gharama zote zitakazohusu ubomoji huo.
Waziri alisema kuwa agizo hilo pia linawahusu wakulima na wafugaji wanaofanya shughuli zao katika vyanzo vya maji.
No comments:
Post a Comment