







MBIO ZA VODACOM ZANOGESHA MSIMU WA KILIMANJARO MARATHON
- ZAVUTIA ZAIDI YA WAKIMBIAJI 7,000
- WAKIMBIAJI WOTE WAPATA ZAWADI YA USHIRIKI KUTOKA VODACOM
Katika mbio hizo zinazofadhiliwa na kampuni ya mawasiliano Vodacom zimevutia wakimbiaji zaidi ya 7,000 na hivyo kuendelea kuwaza kipekee kwa jinsi inavyotoa nafasi kwa makundi mbalimbali kushiriki kama sehemu ya kusherehekea msimu wa mbio za kila mwaka za Kilimanjaro Marathon.
Kupitia mbio hizo za kujifurahisha za Vodacom makundi mbalimbali ya wasio wakimbiaji wa kulipwa yaani 'Proffessional Runners hupata fursa ya kushiriki na kuwa sehemu ya shamrashamra za Kilimanjaro Marathon na pia kutumia nafasi hiyo kunyoosha viungo, kuimarisha afya huku wengine wakitumia mbio hizo kama kipimo cha kujipanga kushiriki mbio ndefu katika mashindano mbalimbali.
Mbio hizo zilianzia eneo la Nje ya Chuo Kikuu cha Ushirika cha Mjini Moshi zikianzishwa na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Ibrahim Msengi na kumalizikia ndani ya uwanja wa mpira wa miguu wa Chuo hicho ambapo washiriki walipata zawadi mbalimbali za ushiriki kutoka kampuni ya Vodacom.
Akizungumzia mbio hizo, Afisa Matukio na Udhamini wa Vodacom, Ibrahim Kaude amesema Vodacom inajivunia kuwezesha kila mmoja kuwa sehemu ya mbio za Kilimanjaro Marathon zinazofanyika kila mwaka.
“Kila Mtanzania na hata asie Mtanzania hususan wasio wakimbiaji wa kulipwa angependa kuwa sehemu ya tukio hili kubwa lenye mvuto na sura ya kimataifa hivyo kwetu sisi kuwezesha hilo ni jambo tunalolifurahia na kulipa kipaumbele kila mwaka.” Amesema Kaude
Kaude amesema katika kuonesha kuwa mbio hizo ni za kipekee na zinafurahiwa na kila mmoja idadi ya washiriki imeongezeka kwa kiasi kikubwa kulinganisha na idadi ya walioshiriki mbio hizo mwaka jana.
Pamoja na kubeba jina la mbio za kujifurahisha lakini mbio hizo zimeonekana kuwa na ushindani mkubwa miongoni mwa washiriki miongoni mwao wakiwa wanafunzi wa shule mbalimbali, taasisi, mashirika ya kitaifa na kimataifa pamoja na wakimbiaji mmojammoja.
Katika kuhakikisha kila mmoja anakuwa sehemu ya mbio hizo baadhi ya watu wameonekana wakikimbia na watoto wao huku wakiwahamasisha kuhakikisha wanamaliza mbio hizo ambapo mshindi wa kwanza alitumia kiasi cha dakika 20.
Kwa upande wa washindi wanaume, Bw. DotoI Kangaa alishika nafasi ya kwanza na Elibariki Buko nafasi ya pili wamesema pamoja na kwamba mbio hizo ni za kujifurahisha bado zimekuwa na ugumu kwa kuwa idadi ya washiriki wenye uwezo wa kukimbia ni kubwa na hivyo kutoa ushindani.
Hata hivyo washindi hao wameipongeza Vodacom kwa kutengeneza mazingira ambayo kila mmoja ana kuwa na nafasi ya kufurahia msimu wa Kilimanjaro Marathon na hivyo kulifanya tukio hilo kuwa na sura halisi ya Kitanzania kwa kuwa kinyume cha hapo ingeshuhudiwa idadi kubwa ya wakimbiaji wa nje wakishiriki katika mbio ndefu.
Mbio hizo zimetoa washindi watano ambao wamezawadiwa zawadi mbalimbali ikiwemo simu za mkononi na fedha taslimu zikiwa na jumla ya thamani ya kiasi cha Shilingi Milioni Tisa.
No comments:
Post a Comment