KASHFA ya kumbaka na kutishia kumuua msichana wa miaka 16
inayomkabili Mbunge wa Urambo Magharibi, Profesa Juma Kapuya (CCM),
imezidi kuchukua sura mpya baada ya serikali kutoa kauli nzito ya kutaka
kumfungulia mashitaka mbunge huyo, Tanzania Daima Jumapili limebaini.
Mashitaka yanayotajwa kumkabili mbunge huyo ambaye amepata kuwa
waziri katika awamu tofauti za uongozi, ni pamoja na ubakaji na kutishia
kuua.
Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova,
aliliambia gazeti hili jana kuwa jeshi hilo halitakuwa na sababu ya
kumuacha mbunge huyo kuendelea kutamba mitaani huku akituma ujumbe wa
vitisho kwa binti wa miaka 16 anayedaiwa kumbaka.
Alisema watachukua hatua za haraka kama mtoto huyo atakwenda
kufungua jalada la kutishiwa maisha katika kituo chochote cha polisi
jijini Dar es Salaam wakati wowote.
Kamishna Kova alisema hadi jana jeshi lake lilikuwa halijapata
malalamiko yoyote kutoka kwa binti anayedai kubakwa na kutishiwa maisha
na Profesa Kapuya, kupitia ujumbe mfupi wa simu ya mkononi iliyosajiliwa
kwa jina la Profesa Kapuya na kuongeza kuwa muda wowote taarifa hizo
zitakapofikishwa polisi wataanza kuzifanyia kazi.
“Sisi Polisi hatuna shamba hapa mjini zaidi ya kukabiliana na
uhalifu… na huyo binti mwambie aje afungue malalamiko yake, tena amuone
RPC yeyote katika mikoa ya kipolisi ya Dar es Salaam na si hili la
kutishiwa tu, hata hilo analosema la kubakwa na sisi tutamuwajibisha
aliyefanya hivyo katika makosa mawili tofauti,” alisema Kamishna Kova.
Wakati Kamanda Kova akisema hawatakuwa na ajizi na tuhuma za kubaka
na kutishia kuua zinazomkabili Profesa Kapuya, habari kutoka Ikulu ya
Rais Jakaya Kikwete zinaeleza kuwa kiongozi huyo wa nchi amekerwa na
kauli ya Mbunge huyo wa Urambo Magharibi kuwa
serikali haiwezi kumfanya
jambo lolote.
Ni kutokana na kauli hiyo mtoa taarifa wetu alisema rais aliagiza
vyombo vya dola kufuatilia kwa karibu sakata hilo na kuhakikisha sheria
inachukua mkondo wake.
Juzi gazeti hili lilinukuu moja ya ujumbe mfupi wa maneno kutoka
katika simu ya Profesa
Kapuya kwenda kwa binti anayedai kubakwa na
Kapuya, sehemu ya ujumbe huo unasomeka kuwa: “Mkiuawa itakuwa
vizuri….itawapunguzia gharama za kuishi, usitake kugombana na serikali
mtoto mdogo kama wewe, sisi ndiyo wenye nchi yetu, mwenye hilo gazeti ni
Mbowe, sasa mwambieni nyumba ya kuishi si mmemuingizia hela leo?
Mnatumika tu bure watu wanaingiza hela nyingi, ila mmenitibua lazima
niwaue wiki hii haitaisha nitapiga kambi kote, jana si wamekuficha,
tuone utalindwa milele, maana washatengeneza hela lazima mvae sanda tu,
hilo sio ombi ni wajibu wenu, mnajitia na nyie mafia watoto siyo, watoto
wetu wanauza unga nani anawakamata? Nani atapingana nasi.”
Pia kwa upande wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), taarifa zinaeleza kuwa
chama hicho kimeamua kumtosa mbunge huyo aliyewahi kuongoza Wizara ya
Elimu na Ulinzi kwa nyakati tofauti baada ya kumtaka aache kukihusisha
chama na kashfa yake ya kubaka.
Mmoja wa viongozi wa CCM aliyezungumza na gazeti hili kwa sharti la
kutotaja jina lake kwa vile siye msemaji wa chama, alidokeza kuwa chama
hicho kilijaribu kulimaliza suala hilo kimya kimya, lakini lilikwamishwa
na Profesa Kapuya mwenyewe kwa kutofika kwenye vikao vya usuluhishi na
binti huyo.
Pia imebainika kuwa baadhi ya wabunge waliokuwa wanataka kumsitiri Profesa Kapuya aliishia kuwaona kama wabaya wake.
“Hapa palipofika ahangaike peke yake, watu walijitahidi kadiri
walivyoweza hili suala limalizike lakini mwenzetu alikuwa mzito
kushirikiana nasi, sasa hakuna anayetaka chama kichafuke zaidi,
amesubiriwa Dodoma na watoto wiki mbili hatokei, hadi watoto
wakashauriwa kwenda kuwaona viongozi wakuu Dar es Salaam,” alisema
kiongozi huyo.
Juzi gazeti hili lilichapisha habari kuhusu mwanafunzi huyo aliyesema
kuwa waziri huyo alimbaka kwenye hoteli moja ya kitalii iliyoko jijini
Dar es Salaam mwaka 2011, na kurudia tena kitendo ndani ya ofisi yake
katika Jengo la Biashara Complex lililoko Mwananyamala Juni 3, 2012
alipoitwa kwenda kuchukua ada kwa mara ya pili.
Kutokana na habari hiyo Profesa Kapuya kupitia kwa wakili wake, Yasin
Memba, alitishia kuliburuza gazeti hili mahakamani endapo halitamwomba
msamaha ndani ya siku saba.
Mbali na kutishia kulipeleka gazeti hili na baadhi ya mitandao ya
kijamii mahakamani pia Profesa Kapuya alikana kumfahamu binti anayedai
alibakwa huku akikanusha kumiliki simu namba 0784993930 ambayo imekuwa
ikitumiwa kuwasiliana naye ikiwemo kumtumia ujumbe mfupi wa maneno (sms)
wa vitisho.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa ni kinyume cha sheria za
Mamlaka ya Mawasiliano nchini mtu kugawa namba iliyosajiliwa kwa jina
lake.
Katika namna ya kushangaza, juzi Kapuya kupitia kwa wakili wake
alidai kwamba simu hiyo aliishaigawa miezi sita iliyopita, hivyo
hahusiki kwa namna moja ama nyingine na tuhuma alizopewa.
Wakati Kapuya akikana kumiliki simu hiyo, Novemba 9, mwaka huu gazeti
hili liliwasiliana naye kupitia namba hiyohiyo anayodai kwamba
alishaigawa miezi sita iliyopita.
Tarehe hiyo, gazeti hili liliwasiliana na mbunge huyo ili
kuthibitisha tuhuma zilizokuwa zikimkabili wilayani Kaliua za kumpiga
makofi kiongozi mmoja wa CCM.
Kapuya kupitia namba hiyo, alitoa utetezi wake ambapo gazeti hili lina sauti yake.
Utetezi wa Kapuya pia unaongeza utata kwa kushindwa kufafanua namna
alivyoweza kugawa namba ya simu iliyosajiliwa kwa jina lake kwa mtu
mwingine, huku ikiendelea kutuma fedha na vitisho kwa binti huyo.
Alilishutumu gazeti hili kuwa lilimhukumu na kuchapisha tuhuma zake
bila kumpa nafasi ya kujitetea kama inavyoelekezwa katika tasnia ya
habari.
“Kwa sababu hiyo, amenielekeza niwapatie siku saba gazeti la Tanzania
Daima, mitandao ya kijamii ukiwemo wa Jamii Forum, Justina John na
Vituko Mtaani, ambao walichapisha habari hiyo, waombe radhi kwa uzito
uleule la sivyo atavishitaki mahakamani,” alisema Memba wakati
akizungumza na waandishi wa habari juzi.
CHANZO NI TANZANIA DAIMA
No comments:
Post a Comment