Jaji
 Mkuu wa Tanzania Mh. Othman Chande (Kulia) akitoa ufafanuzi kwa 
waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini mwaka 
2015. Maadhimisho hayo yanaongozwa na maudhui yasemayo “ Fursa ya kupata
 haki: wajibu wa Serikali, Mahakama na wadau”. Kushoto ni Mh. Hussein 
Kattanga, Mtendaji Mkuu wa Mahakama.
Msajili
 Mkuu wa Mahakama, Ignas Kitus (kulia) akizungumza akifafanua jambo 
wakati Jaji Mkuu wa Tanzania Mh. Othman Chande alipokutana na waandishi 
wa habari kuzungumzia maadhimisho ya Siku ya Sheria leo jijini Dar es 
salaam.
Waandishi wa habari waliohudhuria mkutano huo leo. Picha na Aron Msigwa -MAELEZO.
Na. Aron Msigwa – MAELEZO.
 Rais Jakaya Kikwete anatarijiwa kuwa mgeni rasmi katika kilele cha
 maadhimisho ya Siku ya sheria nchini (Law Day) itakayofanyika Februari 
4, 2015, katika viwanja vya mahakama vilivyopo mtaa wa Chimala jijini 
Dar es salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam, Jaji 
Mkuu wa Tanzania Mh. Othman Chande amesema kuwa maadhimisho hayo kwa 
mwaka huu yanaongozwa na maudhui yasemayo  “ Fursa ya kupata haki: 
wajibu wa Serikali, Mahakama na wadau”.
 Amesema kwa mara ya kwanza maadhimisho hayo yataambatana na 
maonesho ya Wiki ya   Shera yatakayofanyika  katika viwanja vya Mnazi 
Mmoja   kuanzia  tarehe  30 Januari  2015  hadi  tarehe  2 Februari 
 2015 .
Mh.Chande ameeleza kuwa maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini na 
maonesho ya Wiki ya Sheria yanaashiria mwanzo wa shughuli za mahakama 
kwa mwaka 2015  na kufafanua kuwa kipaumbele kitatolewa katika kupunguza
 mrundikano wa mashauri ya muda mrefu yaliyoko mahakamani na 
kushughulikia mashauri yenye mvuto mkubwa kijamii,miradi mikubwa, 
uhujumu uchumi, madawa ya kulevya, Biashara ndani na nje ya nchi na 
Rushwa.
Kuhusu maonesho hayo amesema yanalenga  kutoa elimu kwa wadau wa 
sheria na huduma za kisheria kwa wananchi kuhusu Ufunguaji na uendeshaji
 wa mashauri mbalimbali hasa mirathi, Utatuzi wa migogoro kwa njia ya 
suluhu, kueleza mfumo mpya wa ulipaji wa tozo za kimahakama kwa njia ya 
benki, Kutoa msaada wa kisheria, kutolewa vyeti vya mawakili, kupokea 
maoni na malalamiko kwa ajili ya kuyatafutia ufumbuzi.
Ameeleza kuwa wadau wakuu  watakaoshiriki katika maonesho hayo ni 
Mahakama, Tume ya Utumishi wa Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa 
Serikali, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka, Chuo cha Uongozi wa 
Mahakama- Lushoto, Taasisi ya Mafunzo ya Uansheria kwa vitendo Tanzania 
na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.
Wadau wengine ni Taasisi zinazotoa msaada wa kisheria, TAKUKURU, 
Jeshi la Polisi, Magereza, Chama cha Mawakili Tanganyika na Tume ya 
kurekebisha sheria.
Amesema pamoja na maonesho hayo kutakuwa na matembezi maalum ya 
kuadhimisha Wiki ya Sheria tarehe 1 Februari 2015 yatakayoongozwa na 
Rais mstaafu wa awamu ya pili Mh. Ali Hassan Mwinyi kuanzia Mahakama 
Kisutu kupitia barabara za Serena-Ohio, Gymkana –Obama Road, Mahakama ya
 Biashara, Barabara ya Kivukoni, Sokoine , Railway, Nkurumah, Lumumba na
 Mkunguni hadi Mnazi Mmoja.
 
 
 
 
 
 
 



 
No comments:
Post a Comment