Baada
ya sintofahamu kuhusu uamuzi wa kituo cha polisi Yombo Vituka,
kutochukua malezo ya tukio la kung’atwa na nyani mtoto Abdul Idd (9),
uongozi wa juu wa jeshi hilo umechukua hatua za kulishughulikia.
Abdul aling’atwa na nyani anayedaiwa kuwa
moja ya wanyama pori wanaofugwa na mfanyabiashara mmoja, mkazi wa eneo
la Yombo Lumo jijini Dar es Salaam.
Nyani huyo anadaiwa kutoka nje ya nyumba
ya mfanyabiashara huyo ambaye jina lake halijafahamika, na kuwavamia
watoto walipokuwa wanacheza mpira, miongoni mwao alikuwa Abdul,
aliyevamiwa, kushambuliwa na kung’atwa mkononi.
Hata hivyo, tukio hilo lililoibuliwa na
gazeti hili Jumapili iliyopita, liliwasilishwa kituo cha polisi Yombo
Vituka, lakini askari waliokuwepo siku hiyo, hawakuchukua maelezo kwa
ajili ya kufungua jalada ili mchakato wa kisheria wenye lengo la kudai
haki itendeke.
Badala yake, askari hao walitoa taarifa maalum kupitia fomu namba tatu maarufu kama PF 3 ili mtoto huyo akapate matibabu.
Wazazi wa mtoto huyo, Idd Rashid na Aisha
Suleiman, waliiambia NIPASHE Jumapili kuwa baada ya kuwasilisha taarifa
hizo kwa gazeti hili, walirejea kituoni hapo na kuulizia mchakato wa
kufungua jalada.
Walisema baada ya kudai haki ya
kuchukuliwa maelezo, walijibiwa yalichukuliwa wakati wakihojiwa na
kwamba yaliandikwa kwenye karatasi.
Kisha walipewa kumbukumbu yenye namba RB/1718/2012 ikiwa na kichwa kinachosomeka, “kushindwa kudhibiti mifugo.”
Hata hivyo, wazazi hao wanasema
wanapofuatilia suala hilo polisi, wamekuwa wakijibiwa kuwa mhusika
anayepaswa kuhojiwa, yupo safarini mkoani Morogoro.
“Tukienda wanatuambia kwamba
mfanyabiashara anayefuga wanyama pori ambao polisi wameandika kuwa ni
mifugo, yupo Morogoro, sasa hatujui cha kufanya,” alisema Idd katika
mahojiano na NIPASHE Jumapili juzi.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Temeke, David
Misime, alipowasiliana na NIPASHE Jumapili mwishoni mwa wiki, alisema
ofisi yake inashughulikia mambo mengi, hivyo apewe muda wa kuwasiliana
na Mkuu wa Polisi wilaya ya Temeke.
“Unafikiri mimi nina kila kitu hapa mezani
kwangu, nipe muda nifuatilie kwa kuwasiliana na OCD (Mkuu wa Polisi wa
Wilaya), niongee naye halafu tutawasiliana,” alisema.
Hata hivyo, hadi tunakwenda mitamboni, Misime hakupatikana kuelezea suala hilo.
CHANZO:
NIPASHE JUMAPILI
No comments:
Post a Comment