CHANZO CHA HABARI NA SALUTI5- www.saluti5.com
WENGI wamezipokea kwa mshituko taarifa za kifo cha mwanamipasho Maariam Khamis “Paka Mapepe" (26), aliyefariki wakati wa kujifungua kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam jana alfajiri.
Hiyo
ni kwasababu, Paka Mapepe alikuwa kivutio kikubwa na kipenzi cha wengi,
hasa kutokana na uimbaji wake uliojaa hisia nzito, kwenye tungo zote
alizoimba.Hadi mauti yanamfika, Paka Mapepe alikuwa yu msanii wa kundi la mipasho la TOT Taarab lililop0 chini ya chama tawala CCM.

Alijiunga
na TOT Taarab mwanzoni mwa mwaka jana, akitokea katika kundi la Five
Stars Modern Taarab aliloingia mwishoni mwa mwaka 2009.
Paka
Mapepe aliipa kisogo Five Stars na kuhamishia virago TOT Taarab muda
mfupi kabla ya ajali ya kundi hilo iliyoua wasanii 13, Machi, mwaka
jana, Mikumi Morogoro.
Akiwa Five Stars, alitikisa vilivyo kwa vibao viwili; ‘Ndo Basi Tena’ pamoja na ‘Uzushi Wenu Haunitii Doa’ .
www.saluti5.com iliwahi kuongea naye
wakati wa uhai wake, kuhusiana na msiba wa wasanii wenzake wa Five
Stars, ambako alisema kuwa, ni msiba uliogonga kwa kishindo moyoni
mwake.
Mara
kwa mara alikuwa akiweweseka na kuwaota baadhi ya marehemu wasanii wa
Five Stars, kila alipokumbuka namna alivyoishi nao vema,hata pale
alipobadili upepo na kuingia TOT Taarab.
Historia yake kimuziki ilianzia mwaka 2003, mara baada ya kuhitimu elimu ya sekondari, ambako alipenda sana Taarab, kwa kuvutiwa na magwiji wa mipasho.
Baadhi
ya magwiji hao waliokuwa wakimvutia Paka Mapepe ni pamoja na Zuhura
Shaaban, ‘Malkia wa Mipasho’ Khadija Kopa na marehemu Nasma Khamis
‘Kidogo’.
Wakati
huo, kutokana na shetani muziki kumpanda kindakindaki kichwani kwake,
alikuwa akiandika kwenye daftari mashairi ya baadhi ya vibao vyao na
kuviimba mara kwa mara kila alipotulia.
Kati
ya watu waliogundua mapema kipaji chake cha uimbaji na kukifanyia kazi,
ni baba yake mdogo aitwaye Kessy Abdallah ambaye alimuunganisha kwenye
kundi la Segere No2, jijini Dar es Salaam, ili kujifua zaidi.
Akiwa Segere, ambalo baadhi ya vinara wake alikuwa Mussa Msuba,
alirekodi kibao kiimoja kinachokwenda kwa jina la ‘Mpenzi Wana kabla albamu yake haijatoka, kundi lilisambaratika.
Mwaka
2007, Mussa Mipango, kati ya wacharazaji mahiri wa gitaa zito, Besi
hapa nchini, aliyeko TOT Taarab hivi sasa, alimuunganishia katika kundi
la Zanzibar Stars Modern Taarab ‘Watoto wa Pwani’.
Hakukaa sana Zanzibar Stars kwani mwaka huohuo, 2007 alitimkia East African Melody Taarab alikorekodi kibao ‘Paka Mapepe’ kilichotokea kutikisa vilivyo kiasi cha mashabiki kuamua jina hilo liwe la kwake moja kwa moja.
Mwaka
2008, Paka Mapepe alirejea Zanzibar Stars alikofikia kurekodi kibao
‘Huliwezi Bifu’, kabla ya vingine kama vile; ‘Raha ya Mapenzi’,
‘Narindima Mie’ na ‘Shoga Habari Ndo Hiyo’ .
Kila wakati, Paka Mapepe alikuwa akikiri kuwa, ujuzi wake kiuimbaji ulikuwa unatokana na kutilia mkazo madrasa ya Shadria, jijini Dar es Salaam, alikosoma na kufikisha juzuu mbili.
Mara
tu baada ya kuingia TOT Taarab, Paka Mapepe alipewa kurekodi kibao
‘Sidhuriki na Lawama’, ambacho hata mwenyewe alikuwa akithibitisha kuwa,
kilitokea kumsogeza na mashabiki wengi wa mipasho.
Kati
ya watu ambao mara kwa mara alipenda kuwataja kuwa ni miongoni mwa
waliochangia kumfikisha alipoishia, ni pamoja na baba na mama yake
waliompa moyo tangu alipoanza kujiingiza katika muziki.
Aidha,
alikuwa pia akipenda kuvishukuru vikundi vyote vya muziki wa taarab
alivyopitia ikiwamo Melody na mashabiki pamoja na wapenzi wote kwa
ujumla.
Aliolewa na mcharazaji mahiri wa gitaa la Besi, Haji Kijungu, aliyejaliwa kuzaa naye mtoto mmoja aitwaye Taliq (6).
Paka
Mapepe alizaliwa mwaka 1986, jijini Dar es Salaam na kupata elimu ya
msingi katika shule ya Amana, Ilala kuanzia mwaka 1994 hadi 2000 na
sekondari ya Jamhuri kati ya mwaka 2001 na 2003.
MAZISHI ya mwimbaji Mariam Khamis aliyefariki jana alfajiri yatafanyika leo, Magomeni jijini Dar es Salaam.
MUNGU AMLAZE MAHALA PEMA PEPONI.
No comments:
Post a Comment