CHELSEA itaikaribisha Liverpool katika Uwanja wa Stamford Bridge Jumapili ya leo katika moja ya mechi kubwa za Ligi Kuu England.

Timu hizi zinakutana huku kukiwa na kumbukumbu kuwa Liverpool imeshinda mechi tatu (mbili za Ligi Kuu, moja ya Carling Cup) kati ya nne walizokutana msimu uliopita – mechi pekee waliyoshindwa ni ya fainali ya Kombe la FA.
Liverpool inaonekana kuvutia mchezoni chini ya bosi wao mpya, Brendan Rodgers, lakini bado inashindwa kugeuza mafanikio hayo kuibuka na ushindi katika mechi za Ligi Kuu.
Baada ya mechi 10, imebaki katika nusu ya chini kwenye msimamo wa ligi, ikiwa imeshinda mara mbili tu na kuwa na pointi 11, huku tatizo lao kuu likibaki kuwa upachikaji mabao.
Liverpool imefanikiwa kutikisa nyavu za adui mara 13 pekee, huku saba kati ya hayo yakifungwa na kinara wao wa ushambuliaji, Luis Suarez.
HABARI ZA CHELSEA:
Roberto Di Matteo bado hatarajiwi kuwa na majeruhi Frank Lampard na kuna shaka pia kama Ashley Cole ataweza kuwa fiti kutoka na maumivu ya misuli ya paja aliyopata katika mechi iliyopita nyumbani kwa Swansea, ingawa hali inaweza kumpa nafasi Ryan Bertrand ya kuanza beki ya kushoto.
Hata hivyo, Roberto ana bahati ya kuweza kumtumia tena John Terry baada ya nahodha huyo wa klabu kumaliza adhabu yake ya kukosa mechi nne aliyopewa kutokana na kutenda vitendo vya kibaguzi kwa Anton Ferdinand.
Mbele, kuna matumaini kwa Fernando Torres kuweza kupiga bao lake la kwanza kwa Chelsea dhidi ya Liverpool baada ya kucheza mechi nne mfululizo bila kutikisa nyavu.
Kikosi cha kwanza kwa Chelsea kinatarajiwa kuundwa na Cech, Ivanovic, Terry, Luiz, Bertrand, Mikel, Ramires, Oscar, Hazard, Mata na Torres.
Mchezaji wa kuchunga: Oscar ni mmoja wa wachezaji waliotokea kupiga mabao makali Chelsea, lakini bado ukweli unabaki kuwa yeye si kila kitu. Kinda huyu amekuwa akijitoa kusaidia timu, sasa je, ataweza kupiga bao lake la kwanza katika Ligi Kuu?
HABARI ZA LIVERPOOL
Brendan Rodgers anarudi kwa mara ya kwanza Stamford Bridge, kama kocha wa Liverpool. Hakuna shaka kwamba atakuwa akitafuta kufanya kweli mbele ya mwajiri wake wa zamani (aliwahi kuwa kwenye benchi la ufundi la Chelsea enzi za Jose Mourinho), lakini anakabiliwa na jaribio zito.
Baada ya kupumzisha mastaa kadhaa wenye majina kwenye mechi ya Europa League usiku wa Alhamisi iliyopita, Rodgers anatarajiwa kutumia kikosi madhubuti kwa ajili ya mechi hii.
Anayetarajiwa kurejea kutoka kuwa majeruhi ni beki wa zamani wa Chelsea, Glen Johnson. Hata hivyo mchezaji mwingine wa zamani wa Chelsea, Fabio Borini, yupo kwenye orodha ya majeruhi.
Mchezaji wa kuchunga: Luiz Suarez ni mchezaji mmoja wa Liverpool mwenye uwezo wa kuuweka mchezo kwenye himaya yake. Si kila siku inakuwa njema kwake, lakini akiamka vizuri, anakuwa injinia wa kweli wa ushindi.
DONDOO ZA MECHI NA TAKWIMU:
Kisasi ni kitu kilicho kwenye orodha ya mechi ya Jumapili hii. Liverpool ilifanikiwa kufanya kweli mara mbili dhidi ya Chelsea katika Ligi Kuu msimu uliopita.
Katika siku za karibuni, kitabu cha rekodi kinaonyesha kuwa matokeo yako wazi kwa kila timu – hakuna iliyoachwa mbali. Katika misimu nane iliyopita, timu hizi zimekutana mara 32, huku Chelsea ikishinda mara 13 na Liverpool 12.
RATIBA LIGI KUU ZA ULAYA
ENGLAND
Jumapili, Novemba 11, 2012
Man City v Tottenham, saa 11:30 jioni
Newcastle v West Ham, saa 1:00 usiku
Chelsea v Liverpool, saa 2:00 usiku
HISPANIA
Jumapili, Novemba 11, 2012
Valladolid v Valencia, saa 9:00 alasiri
Bilbao v Sevilla, saa 1:00 usiku
Mallorca v Barcelona, saa 2:50 usiku
Atletico v Getafe, saa 4:45 usiku
Levante v Madrid, saa 6:30 usiku
ITALIA
Jumapili, Novemba 11, 2012
Palermo v Sampdoria, saa 9:30 alasiri
Chievo v Udinese, saa 12:00 jioni
Torino v Bologna, saa 12:00 jioni
Genoa v Napoli, saa 12:00 jioni
Parma v Siena, saa 12:00 jioni
Lazio v Roma, saa 12:00 jioni
AC Milan v Fiorentina, saa 12:00 jioni
Atalanta v Inter Milan, saa 5:45 usiku
Via www.saluti5.com
No comments:
Post a Comment