WAKATI Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameunda tume kuchunguza
matokeo mabaya ya mtihani wa Kidato cha Nne mwaka 2012, Chadema
kimesisitiza msimamo wake kwamba kitafanya maandamano kushinikiza Waziri
wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa na Naibu wake,
Philipo Mulugo wajiuzulu.

Lakini jana Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema watafanya maandamano makubwa aliyoyaita ya kihistoria, katika mikoa ya Mwanza, Arusha, Mbeya na Dar es Salaam ili kushinikiza kutekelezwa kwa hatua hiyo.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Mtatatila, Sumbawanga mkoani Rukwa, Mbowe alisema: “Lengo la maandamano ni kuwataka waziri wa elimu na naibu wake wajiuzulu kwani wameshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo na kusababisha watoto wa maskini kufanya vibaya kwenye mitihani yao.”
Alisema maandamano hayo yatahusisha wafanyakazi wa Serikali, mama lishe na wafanyabiashara wa usafirishaji wanafunzi wa shule za msingi na sekondari... “Siku hiyo hakutakuwa na masomo wala kazi, kila kitu kitasitishwa.”
Mbowe alisema maandamano hayo yatakuwa ya
kihistoria na kwamba Chadema kinataka kuwafungua macho wananchi walio na
kipato cha chini ambao hawana uwezo wa kusomesha watoto wao nje ya nchi
ili washinikize Dk Kawambwa na Mulugo waachie ngazi.
“Tunataka shule za sekondari na msingi zisigeuzwe kuwa vituo vya kulelea watoto, bali vifanye kazi za kutoa elimu, kama ilivyokusudiwa,” alisema Mbowe.
Hata hivyo, Mbowe aliwataka wananchi kuwa makini
na uchochezi unaofanywa na baadhi ya vyama vya siasa, badala yake
waangalie chama chenye sera, mtazamo na harakati za kuleta mabadiliko
yatakayokuwa na manufaa kwa Watanzania wote.
“Njia sahihi ni kuhakikisha mnajiondoa, kwani ili muweze kujua mustakabali wa maisha yenu ni lazima mhakikishe mnakuwa makini kufanya uamuzi ulio sahihi kwa viongozi mnaowataka, ”alisema Mbowe.
Hii ni mara ya pili katika mwaka huu kwa Chadema
kutaka viongozi wajiuzulu. Mwezi uliopita, chama hicho kilimtaka Spika
wa Bunge, Anne Makinda na Naibu wake, Job Ndugai wajiuzulu kwa maelezo
kuwa wamekuwa wakiminya demokrasia, kuubana upinzani na kupendelea chama
tawala (CCM) bungeni.
No comments:
Post a Comment