Mwendesha
Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Uhalifu wa Kimataifa (ICC), Fatou
Bensouda, ametua nchini jana na kufanya mazungumzo na Rais Jakaya
Kikwete, Ikulu Dar es Salaam.

Hatua hiyo ya ICC imekuja ikiwa ni miezi sita tangu Serikali ya Tanzania ilipopelekwa katika mahakama hiyo, iliyoko The Hague, Uholanzi kwa madai ya kukiuka haki za binadamu.
Malalamiko hayo maalumu yalipelekwa ICC na Kituo
cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Septemba 28 mwaka jana, baada ya
kutokea kwa mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa habari wa Kituo cha
Televisheni cha Channel Ten, Daudi Mwangosi na watu wengine 23.
Taarifa ya LHRC ilieleza kuwa pamoja na watu hao kuuawa, Serikali ilishindwa kuwachukulia hatua wahusika.
Mbali na kuishtaki Serikali ICC, kituo hicho cha Sheria na Haki za Binadamu pia kilipeleka mashtaka kwenye Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu.
Mkurugenzi Mtendaji wa kituo hicho, Dk Hellen
Kijo-Bisimba, alisema kuwa walifungua mashtaka hayo ili kuzitaka mamlaka
hizo za kimataifa kufanya uchunguzi na kuichukulia hatua stahiki za
kisheria dhidi ya Serikali ya Tanzania.
Jana Rais Jakaya Kikwete alikutana na Bensouda na kufanya mazungumzo na baadaye walipiga picha za pamoja nje ya Viwanja vya Ikulu, akiwa pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Kairuki na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Eliezer Feleshi.
Katika maelezo yake Bisimba alisema: “Tumepeleka
mashtaka 24 ICC tangu Septemba 28 mwaka huu, ambayo yanahitajika
kufanyiwa uchunguzi na kuchukua hatua kali dhidi ya Serikali ya Tanzania
ambayo imekuwa ikiwalinda viongozi wake wanaokiuka haki za binadamu.”
“Tunatarajia kuona uwajibikaji wa viongozi wote wa Serikali na vyombo vya dola waliohusika kwa njia yoyote ile. Hatua hizo au uwajibikaji huo ni pamoja na kujiuzulu, kuachishwa kazi na kufikishwa Mahakamani,” aliongeza Dk Bisimba.
Gazeti hili lilipomtafuta Jaji Werema kuzungumzia
ujio wa Bensouda alisema kuwa Mwendesha Mashtaka huyo alikuwa mgeni wa
Rais Kikwete, hivyo hawezi kueleza kilichozungumzwa.
“Alikuwa mgeni wa Rais, lakini kubwa nililolisikia
ni kwamba alikuja kusalimia kwa sababu tangu alipoteuliwa hakuwahi kuja
Tanzania,” alisema Werema.
Kama ilivyokuwa kwa Werema, naye Feleshi alikwepa
kuzungumzia ujio huo wa Mwendesha Mashtaka Mkuu wa ICC, huku akisema
jambo hilo linaweza kutolewa ufafanuzi na Ikulu.
LHRC ilichukua hatua hiyo kutokana na kuongezeka kwa mauaji ya
raia wakiwa katika mikono ya vyombo vya dola, huku Serikali ikigwaya
kuwachukulia hatua za kisheria waliohusika.
Pamoja na hatua ya kushtakiwa kwa Serikali katika
mamlaka hizo, Bisimba alisema kuwa bado wanataka kuona viongozi wote wa
Serikali na vyombo vya dola waliohusika kwa namna yoyote na mauaji ya
Mwangosi na raia wengine wakiwajibishwa.
Alifafanua kwamba kuanzia Januari hadi Septemba
mwaka jana, jumla ya watu 24 waliuawa na watendaji wa vyombo vya ulinzi
na usalama.
Dk Bisimba alisema tangu mwaka 2001 hadi sasa, kituo
hicho kimekuwa kikifuatilia kwa karibu matukio mbalimbali ya mauaji
yanayoendelea kufanywa na vyombo vya dola na hakuna hatua
zinazochukuliwa dhidi ya wahusika.
Tayari watu wanne nchini Kenya wamefikishwa ICC
wakikabiliwa na mashtaka ya kuhusika na vurugu zilizosababisha vifo vya
mamia ya watu katika uchaguzi mkuu uliopita nchini humo.
E & P
Dondoo
Dondoo
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Septemba 28 mwaka jana kilipelekwa malalamiko Maalum ICC kuhusu mauaji ya watu 24.
Serikali inalalamikiwa kushindwa kuzuia na
kuwachukulia hatua wanaohusika na mauaji ya watu 24 waliuawa katika
wakiwa mikononi mwa vyombo vya dola.
Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Uhalifu wa Kimataifa (ICC), Fatou Bensoud pamoja mengine kuulizia
No comments:
Post a Comment