Rais Mohammed Mursi wa Misri siku ya jana amefanya ziara hapa Ujerumani ambapo 
amekutana na Kansela Angela Merkel. Mursi alipokelewa kwa gwaride la 
heshima katika ofisi ya Kansela.Wanajeshi walikuwa wamejipanga nje ya ofisi ya Kansela Merkel mjini 
Berlin, kumpokea rais Mohammed Mursi. 

Merkel na mgeni wake walitembea 
katika zulia jekundu huku tarumbeta zikiburudisha. Hii ni mara yake ya 
kwanza kwa Mursi kuitembelea Ujerumani. Baada ya kula chakula cha mchana
 pamoja, Merkel na Mursi walizungumza na waandishi wa habari.
Awali Mursi alikuwa amepanga kubakia Berlin kwa muda wa siku mbili 
lakini hali tete ya usalama nchini mwake imemlazimisha kurejea nyumbani 
leo. Alikuwa amedhamiria pia kuitembelea Ufaransa siku ya Ijumaa, lakini
 safari hiyo imebidi ifutwe.

Mvua ilikuwa inanyesha wakati Merkel na Mursi walipoelekea katika ofisi ya Kansela
Akizungumza na waandishi wa habari, Kansela Merkel alisema 
kwamba anataka kuona mazungumzo yakifanyika na vyama vyote vya kisiasa. 
Pamoja na hayo ameitaka serikali ya Mursi iheshimu haki za binadamu. 
Masuala ya kiuchumi yalizungumziwa pia. "Kwa mtazamo wangu, ukuaji wa 
kiuchumi ni jambo linalowawezesha wananchi kuwa na maisha mazuri. Ni 
muhimu mgogoro wa uchumi uepukwe. Kwa njia hiyo uchumi utasaidia pia 
kuimarisha hali ya kisiasa."
Mbali na mgogoro wa kisiasa unaoendelea, tatizo kubwa linaloikabili 
Misri kwa sasa ni la kiuchumi. Idadi ya watalii imepungua kwa kiasi 
kikubwa baada ya mapinduzi kutokea mwaka 2011. Hivi sasa Misri inahitaji
 wawekezaji kutoka nje. Hapa Ujerumani, wafanyabiashara wanaelewa kwamba
 Misri ni mahala pazuri pa kuwekeza lakini wanahofia hali ya usalama.
Mursi aahidi demokrasia zaidi

Maandamano yaliyoambatana na vurugu katika uwanja wa Tahrir.
Nchini Misri kwenyewe viongozi wa vyama vya upinzani 
wametangaza kuwa tayari kufanya mazungumzo na serikali. Mohammed El 
Baradei ambaye ni kiongozi katika chama cha ukombozi wa kitaifa ametoa 
tangazo hilo siku mbili tu baada ya upinzani kusema kwamba hauko tayari 
kwa mazungumzo.
Katika mkutano wake na Kansela Merkel, rais Mursi ameahidi kuharakisha 
juhudi za kuleta demokrasia nchini mwake, akisema kuwa Misri inataka 
kuwa nchi inayofutata utawala wa sheria. "Misri itakuwa nchi inayoruhusu
 uhuru wa kutoa maoni," alieleza Mursi akiishukuru Ujerumani kwa kuwa 
mshirika wake katika juhudi za kuleta demokrasia.
Kiongozi huyo ametaja pia kwamba yuko tayari kupanua mahusiano baina ya 
nchi yake na Ujerumani lakini akasisitiza kwamba ushirikiano huo 
hautakiwi kuwa kigezo cha nchi moja kuingilia mambo ya ndani ya nchi 
nyingine. Mursi anakutana pia na wawakilishi wa sekta mbali mbali za 
kiuchumi hapa Ujerumani kutafuta wawekezaji.
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment