CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemwandikia barua
kali Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, kikisema kuwa hakiko
tayari kutoa maoni kuhusu vurugu zilizotokea hivi karibuni mjini Dodoma.
Sababu kubwa iliyotajwa na chama hicho ni kwamba suala hilo ni la
kijinai na msajili hana mamlaka ya kushughulikia makosa ya namna hiyo.
Msimamo huo wa CHADEMA unakuja siku chache baada ya Tendwa kupitia
barua yake ya 05/02/2013, yenye Kumb. Na. AB.115/123/01A/45 kumtaka
Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa, atoe maoni yake juu ya
vurugu zilizotokea mwishoni mwa juma lililopita.
Katika vurugu hizo wanachama wa CCM, wakiwemo viongozi, wabunge na
makada waandamizi, waliwavamia na kuwashushia kipigo wanachama na
viongozi wa CHADEMA.
Vurugu hizo zilitokea eneo la Mwanga Bar baada ya wafuasi wa CCM
wakiongozwa na mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Rage, kung’oa mlingoti na
kushusha bendera ya CHADEMA kisha kufanya mkutano wa maadhimisho ya
miaka 36 ya kuzaliwa chama hicho.
CHADEMA katika barua hiyo ambayo imesainiwa na Idara ya Sheria ya
chama hicho kwa niaba ya katibu mkuu wake, yenye Kumb. Na.
C/ADMMSJ/04/04 ya 06/02/2013, wanasema chama hakiwezi kutoa maoni yake,
kwa sababu suala hilo ni la kijinai.
Viongozi wake mkoani Dodoma, wameshafungua mashtaka, hivyo kumtaka
Tendwa awasiliane na mamlaka zinazohusika na makosa ya jinai.
“Nimeagizwa na katibu mkuu nikujulishe kuwa hatatoa maoni kuhusu tukio
lililotokea Dodoma siku ya tarehe Februari 3, 2013 kwa kuwa suala hilo
ni la jinai na viongozi wa CHADEMA Mkoa wa Dodoma, wameshafungua
mashtaka polisi,” ilisomeka sehemu ya barua hiyo.
Batua hiyo inaongeza kuwa kutokana na suala hilo kuwa la jinai, Msajili wa Vyama vya Siasa hana mamlaka ya kulishughulikia.
Vyama vyaweka mkakati
Kufuatia vurugu zinazoendelea kujitokeza kwenye mjadala ndani ya
Bunge kati ya wabunge na kiti cha Spika, vyama vya siasa vyenye
uwakilishi bungeni jana vilikutana chini ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,
na kuweka mikakati ya kumaliza kasoro hizo.
Katika kikao hicho kilichoitishwa na Mwenyekiti wa Kituo cha
Demokrasia Tanzania (TCD), James Mbatia, viongozi wa vyama hivyo
waliziagiza mamlaka husika zitafute mchakato wa kuboresha kanuni za
Bunge.
Lengo ni kuongeza ufanisi, uwajibikaji na uhuru katika kazi za Bunge
na kuhakikisha kuwa kunakuwa na mfumo imara wa kuendesha Bunge la mfumo
wa vyama vingi vya siasa.
Akiwasilisha maazimio hayo ya pamoja, Mbatia alisema viongozi hao
waliazimia kuwepo kwa uvumilivu wa kisiasa baina ya vyama vyao na
wanachama wake katika kutekeleza majukumu yao katika kudumisha amani,
mshikamano na maendeleo endelevu kwa manufaa ya taifa.
Alisema kuwa kuna changamoto mbalimbali kama vile vurugu zilivyotokea
bungeni Februari 2 mwaka huu; kwamba vurugu hizo zinatakiwa kutafutiwa
ufumbuzi wa kina ikiwa ni kujenga mahusiano mema, haki, usawa pamoja na
kasi ya uwajibikaji ndani na nje ya Bunge.
Viongozi wakuu waliohudhuria mkutano huo, mbali na Pinda ni Makamu
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Philip Mangula,
Naibu Katibu Mkuu (CCM) Tanzania Bara, Mwigulu Nchemba, Mbataia
(NCCR-Mageuzi) na Ambar Haji Khamis, Makamu Mwenyekiti (NCCR Mageuzi).
Wengine ni Augustine Mrema na Jeremiah Sherukindo (TLP), Freeman Mbowe
na John Mnyika (CHADEMA), John Cheyo na Izack Cheyo (UDP) na Habib
Mnyaa na Julius Mtatiro (CUF) na wawakilishi wa vyama visivyo na
wabunge, Fahmi Doutwa na Felix Makuwa (UPDP).
No comments:
Post a Comment