Kambi ya Upinzani bungeni imeilaumu serikali kwa kushindwa
kusimamia sheria inayoviagiza vyombo vya utangazaji nchini kuwalipa
wanamuziki kutokana na matumizi ya nyimbo zao.
Akisoma hotuba kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari,Utamaduni na Michezo bungeni mjini Dodoma jana, Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Joseph Mbilinyi (Sugu) alisema, ni aibu serikali kushindwa kuvidhibiti vyombo vya utangazaji ambavyo vimeendelea kuwanyonya wanamuziki kwa kutumia nyimbo zao pasipo kuwalipa hata senti moja.
“Leo hii wasanii wanalazimishwa kuandika barua kuwa wametoa nyimbo zao kwa vyombo hivyo zipigwe bila kulipia na kutokana na mazingira yaliyotengenezwa, wanamuziki wanajikuta ni lazima wahonge! ili nyimbo zao zipigwe ili waweze kupata soko la kazi zao,”.alisema Mbilinyi.
Mbilinyi ambaye pia ni Mbunge wa Mbeya mjini
kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) aliitaka serikali
ianze kwa kuvichukulia hatua vyombo vyake vya utangazaji kwa madai
kwamba vimekuwa mstari wa mbele kukiuka sheria hiyo.
“Ni kejeli kwa taifa, ni kejeli kwa wasanii wanaopata shida kujikwamua kimaisha. TBC leo inapiga na kucheza nyimbo za wasanii bila kuwalipa, huku wizara inayotakiwa kusimamia vyombo hivi inashuhudia sheria zilizopitishwa na bunge hili zinavunjwa,”. alisema Sugu.
Sugu pia aliitaka serikali kusimamia kikamilifu
sekta ya filamu kwa madai kwamba inaweza kuwa chanzo kizuri cha ajira na
kuwaongezea wananchi kipato, sambamba na serikali kukuza uchumi kupitia
kodi.
“Tasnia ya filamu si tu inaweza kuliingizia soko hili fedha bali pia ikipewa thamani ina uwezo mkubwa kwa kutatua tatizo la ajira hapa nchini.
“Kambi rasmi ya upinzani, inaitaka wizara kuja na
takwimu rasmi za ajira zilizotokana na tasnia hii kufikia mwezi Machi
mwaka huu,”.alisema Sugu.Text inakuja hapa.
No comments:
Post a Comment