MFANYAKAZI wa kampuni ya uwekezaji ya Tanzanite One, inayochimba
madini eneo la Mirerani, wilayani Simanjiro, Willy Mushi, ameuawa kwa
kupigwa risasi na watu wanaoaminika kuwa ni wachimbaji wadogo baada ya
kukutana mgodini chini ya ardhi.
Kamanda wa polisi mkoa wa Manyara, Akili Mpwapwa, amethibitisha
kutokea kwa tukio hilo alilosema lilitokea saa 6:00 usiku wa kuamkia
jana na tayari ametuma timu ya upelelezi inayoongozwa na afisa upelelezi
wa mkoa huo, kuchunguza zaidi tukio hilo.
Marehemu alipigwa risasi mbili kifuani upande wa kushoto alipoongozana
na mfanyakazi mwenzake Kennedy Masimbaji kukagua eneo la mgodi
unaoingiliana na migodi ya wachimbaji wadogo.
“Tulipofika kwenye mitobozano ambako kumepangwa mifuko ya viroba vya
mchanga kutenganisha mgodi wetu na ile ya wachimbaji wadogo, ghafla
tukashambuliwa kwa risasi ambazo zote zilimuingia marehemu kifuani na
kufariki papo hapo,” alisema Masimbaji
Mfanyakazi mwingine wa Tanzanite One, Leonard Paul alisema tukio hilo
ni muendelezo wa mashambulizi yanayodaiwa kufanywa na wachimbaji wadogo
dhidi ya wafanyakazi wa mwekezaji pindi wanapokutana chini ya ardhi
ambapo siku kadhaa zilizopita uongozi ulilazimika kusimamisha kazi kutoa
fursa ya polisi kuchunguzi migogoro ya mitobozano.
“Serikali lazima sasa ichukue hatua kuzuia matumizi ya silaha za moto chini ya migodi,” alisema Paul.
Kwa mujibu wa mdogo wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Tumsifu
Mushi, marehemu ameacha mjane na watoto wanne na taratibu za mazishi
zinaendelea.
No comments:
Post a Comment