Habari na Happiness Katabazi wa Tanzania Daima.
MAHAKAMA ya Hakimu  Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imewahukumu 
kwenda jela miaka tofauti washitakiwa  watatu waliokuwa wakikabiliwa na 
kesi ya wizi wa sh bilioni 1.1 katika akaunti  ya madeni ya nje (EPA) 
katika Benki Kuu ya Tanzania.
Hatua hiyo ni baada  ya kuwakuta na hatia katika makosa mbalimbali, 
likiwemo la kughushi hati ya  kuhamisha deni toka Kampuni ya Marubeni ya
 Japan kwenda Kampuni ya  Changanyikeni Residential Complex ya nchini.
Hukumu hiyo ya kesi  ya jinai iliyokuwa ikiwakabili Bahati Mahenge, 
Manase Makalle, Davis Kamungu,  Geofrey Mosha na Edda Mwakale ambaye ni 
mke wa mshitakiwa wa pili, ilitolewa na  jopo lililokuwa likiongozwa na 
Jaji Sekela Mushi, Jaji Sam Rumanyika na 
Hakimu  Mkazi Lameck Mlacha 
ambaye aliisoma kwa niaba ya wenzake.
  Mlacha alisoma  hukumu hiyo kwa kuanza kuikumbusha mahakama kuwa hati 
ya mashitaka ilikuwa na  mashitaka tisa na kwamba kosa la kwanza ni kula
 njama kinyume na kifungu cha  384 cha sheria ya kanuni ya adhabu ya 
mwaka 2002.
Alisema kuwa  washitakiwa hao walitenda kosa hilo kati ya Desemba 23 
mwaka 2003 na Oktoba 26  mwaka 2005, ambapo kwa pamoja na watu wengine 
ambao hawapo mahakamani walitenda  kosa hilo na kuiibia BoT.
Hakimu Mlacha  alisema baada ya kupitia ushahidi na vielelezo vyote, 
mahakama yake inawatia  hatiani Mahenge na Manase na kuwahukumu kwenda 
jela miaka mitano huku  akiwaachia huru washitakiwa wengine.
Katika kosa la pili  la kuwasilisha nyaraka za kutaka kampuni yao ya 
Changanyikeni isajiliwe na  Brela huku wakionyesha jina la kufikirika la
 Samson Mapunda kuwa ndiye  mkurugenzi wa kampuni hiyo, hakimu Mlacha 
pia alisema Mahenge na Manase  walitenda kosa hilo na hivyo mahakama 
yake inawahukumu kwenda jela miaka  mitano.
Kosa la tatu  lilikuwa likimkabili Mahenge pekee akidaiwa kutoa 
nyaraka za uongo za kuomba  usajili wa kampuni zikionyesha Mapunda ndiye
 mkurugenzi wa Changanyikeni, na  hivyo kuwezesha kampuni hiyo kupewa 
usajili na Brela. Mahakama ilimtia hatiani  na kumfunga miaka saba 
gerezani.
Hakimu Mlacha  alilitaja kosa la nne kuwa la Kampuni ya Changanyikeni 
Residential Complex,  ambalo washitakiwa wamejipatia usajili toka Brela 
kwa nia ya udanganyifu kwa  kutumia jina la kufikirika ambapo mahakama 
iliwatia hatiani tena Mahenge na  Manase kwa kuwahukumu kifungo cha 
mwaka mmoja jela.
Katika kosa la tano  la kughushi ambalo linawakabili washitakiwa wote,
 hakimu alisema katika maelezo  ya onyo alilowapa wachunguzi wa kesi 
hiyo, Mahenge alikiri kuwa yeye alikuwa  akitumwa kuchukua hundi za 
malipo ya kampuni hizo mbali na kwamba ndiye  aliyekwenda kupeleka fomu 
Brela za kusajili kampuni yao ya Changanyikeni.
Alisema kuwa  Mahenge alikuwa akisaidiana kufanya kazi hiyo na 
mshitakiwa Manase, hivyo  mahakama hiyo imewatia hatiani Mahenge na 
Manase na Edda ambao ni mke na mume  na kwamba watakwenda jela miezi 18.
Kosa la sita  liliwakabili washitakiwa wote ambalo ni la kughushi hati
 ya kuhamisha deni  lililokuwa likionyesha Kampuni ya Marubeni ya Japan 
imeridhia Kampuni ya  Changanyikeni idai deni lake jambo ambalo si 
kweli.
“Licha upande wa  utetezi kudai hati hiyo ya kuhamisha deni ilikuwa ni
 halisi, lakini sisi kama  mahakama tulipata wasaa tukaikagua kwa 
makini, tukabaini hata hiyo kampuni ya  Marubeni haikutia saini katika 
hati hiyo, na kampuni ya Changanyikeni ilisaini  hati hiyo bila kuwepo 
shahidi wa kushuhudia tukio hilo.
“Hati hiyo  inaonyesha ilisainiwa katika mgahawa wa City Garden Dar es
 Salaam, na  tulijiuliza Marubeni ni kampuni kubwa kwanini haikutia 
saini katika hati hiyo,  na mwisho wake mahakama hii ikakubaliana na 
upande wa jamhuri kuwa hati hiyo  ilikuwa imeghushiwa,” alisema.
Alisema kuwa kwa  kosa hilo, mahakama inawatia hatiani Mahenge na Manase na hivyo wataenda jela  miezi 18.
Shitaka la saba  liliwakabili washitakiwa wote ambalo ni la 
kuwasilisha hati hiyo ya kuhamisha  deni iliyoghushiwa na kwamba 
mahakama yake imemtia hatiani Mahenge ambaye  atakwenda jela mwaka 
mmoja.
Kuhusu shitaka la  nane ambalo ni wizi na shitaka la tisa lilikuwa ni 
la kujipatia kiasi hicho cha  fedha toka BoT, hakimu Mlacha alisema 
mahakama yake inawaachilia huru katika  makosa hayo mawili.
Hata hivyo hakimu  Mlacha alisema ushahidi ulioletwa na upande wa 
jamhuri umeshindwa kuishawishi  mahakama imuone mshitakiwa wa tatu 
(Davis Kamungu) na wanne (Geofrey Mosha)  wana hatia katika kesi hiyo na
 kwa sababu hiyo ikawaachilia huru.
Baada ya hakimu  Mlacha kuwatia hatiani washitakiwa hao, wakili 
Mwanadamizi wa serikali Shadrack  Kimaro alidai upande wa jamhuri hauna 
rekodi za uhalifu za washitakiwa  waliotiwa hatiani ila wanaiomba itoe 
adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine.
Aliomba mahakama  itumie kifungu 384(1) na 358(1) cha Sheria ya 
Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya  mwaka 2002, kuwaamuru washitakiwa 
waliotiwa hatiani kurejesha kiasi hicho cha  fedha serikalini.
Kwa upande wake  wakili wa washitakiwa, Tarimo, aliomba mahakama 
iwapatie adhabu ndogo kwani hii  ni mara yao ya kwanza kukutwa na hatia,
 na kwamba Manase na Edda ni mke na mume  wana familia inawategemea na 
kudai kuwa Edda anasumbuliwa na maradhi ya uzazi  hivyo anaomba wapewe 
adhabu ndogo.
Hakimu Mlacha  alisema amesikiliza maombi ya pande zote mbili na 
kwamba mahakama hiyo inaamuru  Mahenge na Manase warejeshe kiasi hicho 
cha fedha na kwamba adhabu hiyo  itakwenda pamoja.
Kwa maana hiyo  Mahenge peke yake atakwenda jela miaka saba, Manase mitano na Edda miezi 18.
Baada ya hukumu  hiyo kumalizika kusomwa baadhi ya ndugu na jamaa wa 
washitakiwa hao waliangusha  vilio mahakamani hapo na wanausalama 
waliwachukua wafungwa hao na kuwapeleka gerezani.
Novemba 2008,  Wakili Kiongozi wa Serikali Stanslaus Boniface ambaye 
sasa ni marehemu alidai  washitakiwa hao walitenda makosa hayo.
  Hii ni kesi ya tano  sasa ya EPA kati ya kesi 12 zilizofunguliwa 
mahakamani hapo Novemba 2008 na  Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk. 
Eliezer Feleshi kufuatia kumalizika kwa  uchunguzi wa Tume ya Rais 
Jakaya Kikwete ya kuchunguza wizi huo.
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment