Marehemu  Dunia Mzobora enzi za uhai wake.
Rais 
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho 
Kikwete amemtumia Salamu za Rambirambi Waziri wa Habari, Utamaduni na 
Michezo, Mheshimiwa Dkt. Fenella Mukangara kufuatia kifo cha Mwandishi 
wa Habari na Msanifu wa Habari Msaidizi Mkuu wa Gazeti la Uhuru, Bwana 
Dunia Mzobora, kilichotokea tarehe 27 Novemba, 2013 katika Hospitali ya 
Taifa ya Muhimbili (MNH) alikokuwa amepelekwa kwa matibabu ya shinikizo 
la damu.
Marehemu
 aliajiriwa katika Magazeti ya Uhuru na Mzalendo mwaka 1989 kama 
Mwandishi wa Habari Mwanafunzi, kisha akaendelea kupanda ngazi hadi 
kufikia cheo cha Msanifu wa Habari na hatimaye kuwa Msanifu Mkuu 
Msaidizi, cheo alichokuwa akikishikilia hadi mauti yalipomkuta.
“Nimesikitishwa
 na kuhuzunishwa na taarifa za kifo cha mmoja wa Waandishi wa Habari 
Shupavu na Mchapakazi, Dunia Mzobora aliyekuwa akilitumikia Gazeti la 
Chama Cha Mapinduzi (CCM) la UHURU, kilichosababishwa na ugonjwa wa 
shinikizo la damu baada ya kuwa amepelekwa katika Hospitali ya Taifa ya 
Muhimbili kupatiwa matibabu”, amesema kwa masikitiko Rais Kikwete.
Rais 
Kikwete amesema binafsi alimfahamu vyema Marehemu Dunia Mzobora, enzi za
 uhai wake, kama Mwandishi wa Habari aliyejituma vilivyo katika kazi 
zake za kuuhabarisha, kuuelimisha na kuuburudisha Umma kwa kutumia vyema
 kalamu yake, na kwa kuzingatia kikamilifu Maadili ya Taaluma yake ya 
Uandishi wa Habari.
“Kufuatia
 taarifa za kifo cha Dunia Mzobora, ninakutumia wewe Waziri wa Habari, 
Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Dkt. Fenella Mukangara na Wafanyakazi 
wote wa Kampuni ya Magazeti ya Chama ya Uhuru na Mzalendo na kwa kweli 
Waandishi wote wa Habari nchini, Salamu zangu za Rambirambi kwa 
kumpoteza mmoja wa Waandishi wa Habari Mahiri ambaye amelitumikia vyema 
Taifa lake kupitia Tasnia ya Habari”.
“Aidha
 kupitia kwako, naomba unifikishie Salamu zangu za Rambirambi na pole 
nyingi kwa Familia ya Marehemu Dunia Mzobora kwa kumpoteza Baba, 
Kiongozi na Mhimili wa Familia”.
Rais 
Kikwete amewahakikishia Wanafamilia kuwa yeye binafsi yuko pamoja nao 
katika kuomboleza msiba wa mpendwa wao, na anamuomba Mwenyezi Mungu, 
Mwingi wa Rehema aipokee na kuilaza Mahala Pema Peponi Roho ya Marehemu 
Dunia Mzobora, Amina.
Rais 
Kikwete amewaomba wawe na moyo wa uvumilivu, utulivu na subira katika 
kipindi hiki kigumu wanachopitia baada ya kumpoteza mtu muhimu aliyekuwa
 kiungo cha Familia yao, kwani yote ni Mapenzi yake Mola.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
 
 
 
 
 
 
 

 
No comments:
Post a Comment