Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
MSHAMBULIAJI
wa Azam FC, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ anatakiwa kuwa nje kwa wiki
mbili au tatu kuanzia leo kutokana na matatizo ya misuli- maana yake
hatacheza mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga SC Jumapili Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam.
Meneja
wa Azam FC, Jemadari Said Kazumari ameiambia BIN ZUBEIRY leo asubuhi
kwamba, Bocco aliyeumia kwenye michuano ya Kombe la Kagame mwezi
uliopita mjini Kigali, Rwanda baada ya kufanyiwa vipimo, ametakiwa
kupumzika ili kupona vizuri.
“Tuna
majeruhi wawili ambao hawatakuwepo kwenye programu ya mchezo wa Ngao ya
Jamii, ambao ni beki Waziri Salum na Nahodha wetu, John Bocco,”amesema
mshambuliaji huyo wa zamani wa Kariakoo United ya Lindi.
Bocco
aliuamia katika mchezo wa Robo Fainali Kombe la Kagame dhidi ya El
Merreikh ya Sudan ambao Azam FC ilitolewa kwa penalti baada ya sare ya
0-0 ndani ya dakika 90.
Jemadari
amesema kwamba, Azam FC itaingia kambini jioni ya leo katika hosteli za
Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam kuelekea mchezo huo wa Ngao ya
Jamii.
Wachezaji
wengine wote wapo fiti na wamekuwa wakiendelea na mazoezi Uwanja wa
Azam Complex na wanatarajiwa kuingia kambini leo.
Mabingwa
hao wa Tanzania Bara wanaonolewa na kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog
watamenyana na washindi wa pili, Yanga SC walio chini ya kocha Mbrazil,
Marcio Maximo Jumapili Uwanja wa Taifa.
Yanga
SC nayo inatarajiwa kuingia kambini leo kwa ajili ya mchezo huo, ambao
unatarajiwa kuwa marudio ya mchezo wa Ngao ya Jamii mwaka jana timu
zilipokutana tena Uwanja wa Taifa.
Hii
itakuwa mara ya tatu mfululizo, Azam FC kucheza mechi ya Ngao ya Jamii
na mara zote ikifungwa kwanza na Simba SC na baadaye na Yanga SC- lakini
safari hii kocha Omog anataka kupindua matokeo hayo.
Yanga
SC ndio washindi mara nyingi zaidi wa Ngao, mara ya kwanza wakitwaa
mwaka 2001 walipoifunga mabao 2-1 Simba SC, enzi hizo Ligi Kuu
inadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia ya Safari
Lager.
Baada ya hapo, haikuchezwa tena mechi ya Ngao hadi mwaka 2009 wakati Mtibwa Sugar ilipoilaza 1-0 Yanga SC.
Mwaka
2010 Yanga walirejesha Ngao kwenye himaya yao, baada ya kuwachapa tena
wapinzani wao wa jadi, Simba kwa penalti 3-1 kufuatia sare ya bila
kufungana ndani ya dakika 90.
Simba
SC walitwaa mara mbili mfululizo Ngao na kufikia rekodi ya watani,
kwanza 2011 walipoifunga 2-0 Yanga na 2012 walipotoka nyuma kwa 2-0 na
kuilaza Azam 3-2.
Mwaka
jana, Yanga SC ikaweka rekodi ya kuwa timu iliyotwaa mara nyingi zaidi
Ngao ya Jamii, baada ya kuilaza 1-0 Azam FC, bao pekee la kiungo Salum
Abdul Telela ‘Master’.
Na
mwaka huu, tena Azam FC na Yanga SC zinarudia mechi ya Ngao ya msimu
uliopita, zitakapokutana tena Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment