
MTOTO Salma Omary (3) mkazi wa Banda Mbili, Sombetini jijini hapa, anaishi kwa mateso makali baada ya kuzaliwa akiwa hana sehemu ya haja kubwa, hali iliyolazimu kujisaidia kupitia tundu lililotobolewa tumboni kwake.Mama mzazi wa mtoto huyo, Mariamu Andrea (28) aliliambia gazeti hili kuwa zinahitajika kiasi cha shilingi milioni moja ili aweze kutibiwa katika hospitali ya KCMC mjini Moshi na kuwa mzazi mwenzake alimkimbia baada ya kubaini tatizo hilo.
Akiwa anaishi nyumba ya udongo na kulala kwenye kitanda kisicho na godoro, Mariam alisema alikuwa akifanya kazi za ndani katika miji ya Dar es Salaam na Arusha kabla ya kukutana na mwanaume aitwaye Omary, aliyempa ujauzito lakini akamtelekeza baadaye.
“Niliamua kwenda hospitali ya rufaa KCMC kuwaomba wanisaidie lakini waliniambia nitafute fedha, kwani kila ninapoenda natakiwa kulipa shilingi 200,000,” alisema.
Diwani wa kata ya Sombetini, Ally Bananga na Mwenyekiti wa umoja wa wanawake chadema (BAWACHA), Cecy Ndossi wamemkabidhi msaada wa shilingi 500,000 ikiwa ni sehemu ya fedha zinazohitajika kufanyiwa upasuaji.
Kwa anayeguswa na tatizo la mtoto huyu na anajisikia kusaidia wasiliana na mama yake kupitia namba 0767631933.
No comments:
Post a Comment