Wakaidi amri ya mahakama, wasema watafia jela.
HATIMAYE madaktari nchini jana walianza mgomo usio na kikomo kwa
lengo la kuishinikiza serikali kuwatimizia matihaji yao ikiwamo
kuboresha mazingira ya kufanyia kazi pamoja na kuwapandishia mishahara.
Uamuzi huo wa madaktari unapingana na amri ya Mahakama Kuu Tanzania,
Kitengo cha Kazi ambayo juzi ilizuia mgomo huo baada ya kupokea maombi
namba 73 ya 2012 yaliyowasilishwa chini ya hati ya dharura na
Mwanasheria Mkuu wa Serikali dhidi ya Chama cha Madaktari Tanzania
(MAT).
Mahakama hiyo ilitoa amri ya kusitisha mgomo huo mpaka hapo shauri la
pande zote mbili (Serikali na Chama cha Madaktari Tanzania (MAT)
litakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mahakama hiyo iliyotolewa juzi jioni na
kusambazwa kwenye vyombo vya habari, imewataka MAT na wanachama wake
kutoshiriki kwenye mgomo huo.
Mgomo waanza
Katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili iliyopo jijini Dar es Salaam
huduma za dharura zinatarajiwa kusitishwa wakati wowote kuanzia sasa.
Mgomo huo unaanza wiki mbili baada ya madaktari hao kuitaka serikali
itekeleze madai yao la sivyo jana wangeanza mgomo usio na kikomo.
Tanzania Daima Jumapili, lilitembelea hospitali za Jiji la Dar es
Salaam ikiwemo Muhimbili na zile za mkoa ambazo ni Temeke, Amana na
Mwananyamala na kushuhudia kusuasua kwa huduma.
Vitengo vya dharura katika hospitali hizo viliendelea kupokea wagonjwa
huku baadhi ya madaktari wakiweka wazi kuwa kuna uwezekano wa huduma
hizo kusimama katika muda wa saa 24 kuanzia jana.
Muhimbili
Katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili wagonjwa walilamikia huduma
zilizokuwa zikitolewa huku wengine wakisema wametelekezwa na wauguzi
waliokuwa zamu.
Eneo la mapokezi baadhi ya askari walionekana wakiwaeleza wagonjwa
waliofika kuwa huduma zimesimama na kuwasihi waondoke eneo hilo.
Mgonjwa mmoja ambaye alionekana kuchanganyikiwa alisikika akisema kuwa
alimkabidhi nchi Rais Jakaya Kikwete lakini haieleweki kiongozi huyo
anakoipeleka.
“Rais Kikwete nilikukabidhi nchi hii sasa unaipeleka wapi?” alisikika akisema.
John Kobelo, alisema kuwa tangu juzi kijana wake alitakiwa kufanyiwa
upasuaji lakini ilipofika jana aliambiwa ampatie mgonjwa wake chakula
kutokana na huduma hiyo kutokuwepo.
“Kwa kweli hali inasikitisha na kukatisha tamaa, sijui nchi hii
tunaelekea wapi maana viongozi wanaamua kwa makusudi kuchezea uhai wa
Watanzania,” alisikika baba mmoja akilalamika.
Tanzania Daima Jumapili ilifika katika wodi ya Sewa Haji na kukutana
na mgonjwa ambaye hakuwa tayari kutaja jina lake lakini alilalamikia
kitendo cha madaktari kushindwa kupita zamu kwa siku ya jana huku huduma
zikiwa zimezorota.
Katika wodi ya Kibasila gazeti hili lilikutana na baadhi ya wanajeshi
wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambao walikuwa
wakiangaika kumhamisha mgonjwa wao aliyekuwa akilalamika kwa maumivu
makali.
Gazeti hili halikuishia hapo kwani lililazimika kufika katika Kitengo
cha Mifupa (Moi) ambapo ilikutana na Ofisa Uhusiano wa hospitali hiyo,
Jumaa Almasi, ambaye alisema kuwa kwa jana ilikuwa ni vigumu kuzungumzia
mgomo huo kutokana na kuwa siku ya mapumziko.
“Unajua kwa (leo) yaani jana siwezi kuzungumzia mgomo kwa kuwa tuna
kliniki mbili za binafsi, labda picha kamili ya kuwepo kwa mgomo
tunaweza kuipata kuanzia Jumatatu, kwa vile kuna kliniki zote,” alisema.
Aidha, Ofisa Habari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Aminiel
Aligaesha, alijikuta akishindwa kutokea katika kikao cha waandishi wa
habari alichokiita ofisini kwake.
Mwananyamala na Temeke
Hali ilikuwa si shwari kwani baadhi ya wagonjwa walisikika wakisema
kuwa hawajapata huduma na baadhi ya wauguzi wanajifanya kutoa huduma
baada ya kuona wanahabari.
Katika Hospitali ya Amana, Tanzania Daima Jumapili ilishuhudia
shughuli za matibabu zikiwa zinaendelea ingawa baadhi ya wagonjwa
walikuwa wakilalamika kukaa muda mrefu pasipo kupatiwa huduma.
Mmoja wa watu waliokuwa hospitalini hapo aliyempeleka ndugu yake
kupatiwa huduma baada ya kupata ajali aliliambia Tanzania Daima Jumapili
kuwa wamekaa katika eneo hilo zaidi ya saa tatu bila mgonjwa wake
kupatiwa matibabu.
“Nipo hapa na huyu afande tumemleta mtu aliyepata ajali maeneo ya
Sitakishari lakini hatujahudumiwa mpaka saa hizi sasa sijui ndiyo
wanagoma kisirisiri?” alisema mtu huyo aliyeomba jina lake lihifadhiwe.
Katibu wa utawala wa hospitali hiyo, Tunu Mwachale, alisema madaktari
waliotakiwa kufika zamu kwa siku ya jana wote walifika na kwamba
walikuwa wakiendelea na kazi kama kawaida.
Dk. Ulimboka anena
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka, alisema
hawajapata taarifa zozote kutoka Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, ya
kuzuia mgomo huo.
Alisema mgomo ulioanza jana haukihusishi Chama cha Madaktari nchini (MAT).
Alisema wao taarifa hizo wamezisikia katika vyombo vya habari hivyo
hawajui kama zinawahusu wao au MAT, na kwamba itakuwa ni vigumu kutolea
ufafanuzi jambo lisilowahusu.
Dk. Ulimboka alisema kuwa kimsingi serikali imekuwa ikipotosha dhana
nzima ya mgomo huo kwani inaonyesha kuwa suala la posho ndilo
linalogomewa na madaktari wakati si kweli.
“Watu wanadhani tunapigania posho zaidi, hapana tunapigania huduma
bora kwa wagonjwa, kwa sababu sifa ya kwanza katika hospitali ya rufaa
ni kuhakikisha yale yanayoshindikana katika hospitali nyingine
yanawezekana katika hospitali za rufaa,” alisema.
Alitolea mfano kifaa cha kupimia cha CT- SCAN ambacho kina zaidi ya
miezi saba hakifanyi kazi katika Hospitali ya Muhimbili huku ikiwalazimu
baadhi ya wagonjwa wanaofika kutakiwa kufanya kipimo hicho katika
hospitali nyingine.
“Wengine hawana uwezo huo, wale wanaobahatika kufika huku wanakuta
kifaa hakifanyi kazi, huyu ni mgonjwa bado unamuongezea gharama
nyingine, tukiyasema haya wanasema sisi hatuwajali wagonjwa,” alisema
Dk. Uliomboka.
Alisema madai mengine ni pamoja na miundombinu ya hospitali kwa kile
alichoeleza haziwiani na idadi ya wagonjwa na kutolea mfano wodi ya
watoto katika Hospitali ya Temeke kuwa mazingira ni magumu.
Alibainisha kuwa kitaaluma ni lazima wawahudumie wagonjwa wakiwa
vitandani na inapotokea wagonjwa wakiwa chini inawawia vigumu
kuwahudumia, na kwamba hayo ndiyo masuala waliyokuwa wanalalamikia.
“Kwanini hospitali zetu ziwe sehemu ya mateso kwa wagonjwa badala ya
kuwa sehemu ya faraja? Tunaambiwa tuwaandikie dawa wagonjwa, wakienda
dirishani hata Panadol hakuna, haya hawataki kuzungumzia, wameamua
kupandisha posho ya maiti wakati hata katika madai yetu hatukuwa na dai
hilo,” alisema.
Matabibu asili wanena
Chama cha Utabibu wa dawa za asili Tanzania (ATME) wamewataka
madaktari nchini kutopoteza uhai wa binadamu wenzao kama njia ya
kuishinikiza serikali kusikiliza na kuwatekelezea madai yao.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa chama hicho, Simba
Abrahaman, alisema kuwa kwa kufanya hivyo ni kuwanyima haki wagonjwa ya
kupata matibabu.
Abrahaman aliwataka madaktari kukaa meza moja na serikali katika
kuweza kutatua malalamiko yao na si kugoma ambapo anayeathirika ni
mwananchi kwa kukosa haki hiyo ya huduma za afya.
Aidha, katika kuhakikisha mgogoro kama huo hautokei tena siku za
usoni, alisema ni vema kukaundwa mfuko wa afya ambapo wananchi wataweza
kuuchangia, kwa kuwa ukweli ni kwamba wamekuwa wakiitikia kuchangia
mambo mbalimbali ikiwamo vyama vya siasa, hivyo halitakuwa zito.
Chanzo cha hii habari ni Tanzania Daima la 24/6/2012 (LEO JUMAPILI)
No comments:
Post a Comment