Wataka iundwe tume huru ya kuchunguza sakata zima
CHAMA cha Madaktari Tanzania (MAT), kimepanga kufanya maandamano
makubwa ya amani jijini Dar es Salaam ili kupinga dhuluma na uonevu
dhidi ya taaluma muhimu ya udaktari na madaktari wenyewe.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu
wa MAT, Dk. Rodrick Kabangila, alisema maandamano hayo yatatanguliwa na
mkutano mkubwa wa madaktari wote utakaofanyika leo kujadili mustkabali
na mwenendo wa taaluma ya udaktari.
Kwa mujibu wa Dk. Kabangila, MAT inasikitishwa na dhuluma hiyo kwa
kuzingatia uwiano duni wa madaktari hapa nchini ambapo daktari mmoja
hutibu wagonjwa 30,000 kwa mwaka chini ya viwango vya kimataifa.
Alisema jumla ya madaktari 400 walio chini ya usimamizi wa madaktari
bingwa, wamesitishiwa usajili wao na wengine kusimamishwa kazi bila
kujali umuhimu wao kwa mustakabali wa taifa na wananchi wake.
“Tutafanya maandamano ya amani, madaktari wote na wadau wa sekta hii
wenye mapenzi mema tunawaomba washiriki… madaktari tutavaa makoti yetu
meupe na watakaoshiriki nasi wavae vitambaa vyeupe.
Maandamano yataanzia nje ya Hospitali ya Taifa Muhimbili, tutaishia
kwenye geti la Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, tukiwa na mabango ya
kulaani kitendo cha kutekwa, kupigwa na kutelekezwa kwenye msitu wa
Pande alichofanyiwa Dk. Steven Ulimboka,” alisema.
Dk. Kabangila alisema kuwa wataishinikiza serikali iunde tume huru kwa
ajili ya kuchunguza suala la Dk. Ulimboka itakayofanya kazi haraka na
wahusika wote wafikishwe kwenye vyombo vya sheria.
Awali, katibu huyo alieleza kushangazwa kwake na wanaojiita viongozi
wa dini ambao huwakatisha tamaa kwa kuwanena mabaya bila kujali
mazingira magumu wanayofanyia kazi madaktari.
Interns wanena
Kwa upande wake, mwakilishi wa madaktari wanafunzi wa mafunzo kwa
vitendo (interns), Frank Kagoro, alisema kitendo cha Baraza la Madaktari
kusitisha usajili wao bila kuwasikiliza ni kinyume cha matakwa ya
sheria.
Dk. Frank alisema usitishwaji wa usajili huo umefanywa kimakosa kwa
sababu umewagusa waliomaliza mafunzo yao na waliokuwa kwenye likizo ya
uzazi jambo linalowashangaza.
Alisema kuwa kuwafukuza madaktari wanafunzi na kuwaacha madaktari
bingwa ni kosa kwa sababu wanafanya kazi chini ya uangalizi wa mabingwa
hao huku akisisitiza kwamba bila baraza hilo kuwa huru haki za madaktari
zitaendelea kukandamizwa.
“Tunasikitishwa na utendaji wa baraza hili ndiyo maana moja ya madai
yetu hata Waziri Mkuu tulimwambia tunataka baraza huru lisiwe chini ya
Wizara ya Afya. Hapa tunapozungumza baadhi ya madaktari wameanza
kuandika barua za kuacha kazi,” alisema.
Dk. Frank alisema wanaiomba serikali idhamirie kwa dhati kumaliza
mgogoro huu vinginevyo ukandamizaji wanaofanyiwa utawakatisha tamaa hata
wanaotamani kuwa madaktari siku zijazo.
Mgogoro kati ya madaktari na serikali ulianza mwaka 2005 ambapo madai
ya wataalam hao ni mazingira bora ya kazi, vitendeakazi bora, mashine za
kisasa na nyongeza ya posho na mishahara.
Kushindwa kumalizika kwa mgogoro huo kulisababisha Jumuiya ya
Madaktari nchini, kuitisha mgomo mwanzoni mwa mwaka huu ili kuishinikiza
serikali kutimiza madai yao.
No comments:
Post a Comment