MBUNGE wa Mpanda Mjini, Said Arfi (CHADEMA) amewashambulia 
mawaziri wa Wizara ya Uchukuzi kwa madai kuwa wanatoa majibu ambayo 
hayakidhi viwango.
  Kauli hiyo aliitoa jana bungeni alipokuwa akiuliza maswali ya nyongeza
 kwa kuitaka serikali itoe majibu ya kuwaeleza Watanzania hususani wa 
Mpanda ni kwanini stesheni ya eneo hilo haina nyumba ya kusubiria gari 
moshi (treni) wala choo.
Mbunge huyo pia aliitaka serikali ieleze ni lini safari za garimoshi 
zitaanza kutolewa kila siku ili wananchi waepukane na usumbufu wa 
kuuziwa tiketi kwa kulanguliwa.
  Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Sabrina Sungura (CHADEMA) alitaka 
serikali kutoa kauli bungeni ni lini itajenga jengo la stesheni ya reli 
Kigoma kutokana na jengo hilo kuwa katika hali mbaya na linaweza 
kuanguka muda wowote.
Mbunge huyo alisema kuwa licha ya kuwa Kigoma ni sehemu ya kihistoria 
kwa kutumia stesheni hiyo, lakini cha ajabu jengo hilo linavuja.
  Awali katika swali la msingi, Arfi alitaka kujua ni lini serikali 
itajenga jengo la Shirika la Reli lenye hadhi katika stesheni ya reli 
Mpanda.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Charles Tizeba, alisema 
serikali ina nia njema ya kuboresha miundombinu ya shirika hilo yakiwemo
 majengo ya stesheni zote nchini.
  Tizeba, alisema kuwa, kwa sasa serikali inatafuta fedha ili 
kuhakikisha wanajenga kituo cha stesheni ya Kigoma ili kuendelea 
kukifanya kuwa cha kihistoria.
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment