HESABU za timu ya soka ya wanawake, Twiga Stars, kucheza fainali
za Afrika kwa mara ya pili, jana zilitoweka baada ya kufungwa bao 1-0
na Ethiopia kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Licha ya kuhitaji walau ushindi wa bao moja tu kujitwalia tiketi ya
kucheza fainali hizo nchini Guinea ya Ikweta, Twiga Stars wamekubali
kipigo.
Kwa bao hilo moja likifungwa dakika ya 63 na Berkhatawit Girm,
Ethiopia imetwaa tiketi ya fainali hizo kwa ushindi wa jumla ya mabao
3-1.
Katika mechi ya kwanza iliyopigwa wiki mbili zilizopita mjini Addis Ababa, walishinda 2-1.
Berkhatawit alifunga bao hilo baada ya kumtoka beki Fatma Khatib aliyeanguka kutokana na kushikwa na msuli.
Bao hilo lilifungwa dakika moja tu tangu Kocha Charles Boniface Mkwasa
afanye mabadiliko akimtoa Fatma Mustafa na kuingia Ester Chabruma
‘Lunyamila’.
Kabla ya bao hilo, dakika za 19, 31 na 36 na 44, mabeki wa Twiga Stars
walifanya kazi ya ziada kuokoa mashuti hatari ya Ethiopia.
Dakika ya 25, nahodha wa Twiga Stars, Sophia Mwasikili, nusura afunge
bao kwa mpira wa adhabu baada ya Asha Rashid kuchezewa vibaya.
Katika mechi hiyo, Ethiopia walitawala kwa kiasi kikubwa
wakiwalazimisha Twiga Stars kucheza soka ya kulinda zaidi kutokana
mashambulizi makali.
Licha ya Twiga Stars kucharuka kipindi cha pili kwa lengo la kupata
bao, Ethiopia walicheza kwa kujiamini, wakishambulia na kulinda lango
lao.
Hadi filimbi ya mwisho, Ethiopia wakawa washindi wa bao hilo moja, hivyo kujitwalia tiketi ya fainali hizo.
Baada ya mechi hiyo, baadhi ya mashabiki wamelalamikia kiwango duni cha timu hiyo, wakielekeza lawama kwa benchi la ufundi.
Kwa mujibu wa wadau hao, mbali ya Mkwasa kushindwa kupanga kikosi cha
ushindi, pia hata mfumo wa uchezaji, haukuwa mzuri, huku akishindwa
kubadili mchezo hata baada ya kuzidiwa.
Twiga Stars: Fatma Omary, Fatma Khatib, Pulkeria Chalaji, Flora
Kayanda, Sophia Mwasikili, Mwapewa Mtumwa, Amina Ally, Eto Mlenzi, Fatma
Mustafa, Asha Rashid ‘Mwalala’ na Mwanahamis Omary ‘Gaucho’.
Ethiopia: Liya Shibru, Buzhan Endale, Indnshet Tsegaye, Truanche
Mengesh, Henot Dengisho, Berkhatawit Girm, Eden Shiferaw, Zulka Juhad,
Shetaye Sisay, Birtukan Gebrekirsto na Erehma Zerga.
Habari na Clescencia Tryphone
No comments:
Post a Comment