Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeibuka na mkakati mpya 
wa kushika hatamu za dola katika uchaguzi, baada ya kutangaza kufanya 
mabadiliko makubwa ya uongozi na utendaji wake kwa kupeleka mamlaka ya 
makao makuu ya chama kwenye kanda 10; nane zikiundwa Tanzania Bara na 
mbili visiwani Zanzibar.
Mkakati huo, ambao ni sehemu ya utekeyake ya majimbo, ulitangazwa na 
Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, alipofungua mkutano wa 
dharura wa Baraza Kuu la Chama hicho, jijini Dar es Salaam jana, 
ulioitishwa kwa lengo la kujadili mikakakti ya uendeshaji wa shughuli za
 chama kwa ajili ya mustakabali wa chama.
Alisema uamuzi huo umefikiwa ili kuondokana na mazoea yaliyopo 
serikalini ya kung’ang’ania kila kitu kufanywa na kikundi cha watu 
wachache jijini Dar es Salaam.
Alisema Chadema imeamua kuuvunja mwiko huo kwa kuwa ni chama, ambacho 
kinathaminiwa na Watanzania wote, hivyo akawataka wanaChadema kuishi kwa
 kauli zao.
“Kwa hiyo, madaraka ya chama yanatoka makao makuu sasa yanakwenda kwenye
 kanda. Chama kimekua. Ukienda kila mkoa kipo. Hatuwezi kung’ang’ania 
Dar es Salaam tu. Chama sasa kipelekwe kwenye kanda zenu,” alisema Mbowe
 na kuongeza:
“Baada ya kazi kubwa iliyofanywa na makao makuu (ya Chadema) kwa miaka 
20, lazima kama chama siasa tujipange kama dola. Tunakwenda kutawanya 
chama kwenye kanda 10. Tunakwenda na vikosi 10. Tutapeleka magari, 
pikipiki.”
Alisema kazi ya kuchukua dola si ya Mbowe wala ya (Makamu Mwenyekiti wa 
Chadema Tanzania Bara, Said) Arfi) peke yake, bali ni ya wote.
Alizitaja kanda hizo kuwa ni Ziwa Magharibi, ambayo itahusisha mikoa ya 
Mwanza, Geita na Kagera); Kanda ya Ziwa Mashariki (Mara, Simiyu na 
Shinyanga) na Kanda Magharibi (Kigoma, Tabora, Katavi na Rukwa).
Kanda nyingine ni ya Kati (Singida, Dodoma na Morogoro); Kanda ya Nyanda
 za Juu Kusini (Iringa, Njombe, Mbeya na Ruvuma); Kanda ya Kusini (Lindi
 na Mtwara) na Kanda ya Mashariki (Dar es Salaam na Pwani). Nyingine ni 
Kanda ya Kaskazini (Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara); Kanda ya 
Pemba (mikoa yote ya Pemba) na Kanda ya Unguja (mikoa yote ya Unguja).
Alisema katika kila kanda kutakuwa na ofisi na kwamba, chama kitagawa 
vitendea kazi vyote muhimu, yakiwamo magari na pikipiki ili kurahisisha 
na kufanikisha shughuli za chama.
Mbowe alisema kila kanda ina maofisa wenye uzoefu wa kukisimamia chama 
na zitajumuisha pia wabunge wa maeneo husika. Alisema wamefikia uamuzi 
huo ili kukataa malalamiko, ambayo yamekuwa yakitolewa muda mrefu kuhusu
 kila kitu kufanywa na makao makuu ndiyo maana wameamua kuyashusha chini
 mamlaka yake.
Mbowe alisema sababu nyingine, ni kujipanga kwa ajili ya uchaguzi, 
kuanzia ule mdogo wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji na uchaguzi 
mkuu na pia kudhibiti wagombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupita bila 
kupingwa katika uchaguzi.
“Tatizo kubwa la nchi hii ni watu kukaa makao makuu wakifikiri kuwa 
wanajua kuliko wote, wanajua mali kuliko wengine,” alisema Mbowe. 
Alisema yanayotokea mkoani Mtwara ni mwanzo unaoashiria kwamba, wananchi
 hawana imani na serikali na kusema jambo hilo la kujisifu, lakini 
linastahili kupongezwa kutokana na ujasiri unaoonyeshwa na wananchi wa 
mkoa huo.
Mbowe alisema msimamo wa Chadema kuhusu gesi ya Mtwara, iko pamoja na wananchi.
 “Kama CCM wanafikiri ngoma imeishia Mtwara wangoje, kama ni noma na iwe
 noma. Wajiandae kutoa majibu kuhusu dhahabu, mafuta, uranium, twiga, 
pembe za ndovu na rasilimali za nchi,” alisema Mbowe.
Aliitaka serikali kusitisha mara moja mpango wa kuisafirisha gesi kutoka
 Mtwara kwenda Dar es Salam hadi hapo itakapokaa na wananchi, wajadili, 
waridhie na suala hilo lifanyike kwa maslahi ya wote.
Aliitaka pia serikali kuiweka hadharani mikataba yote 26 ya gesi.
Alisema Chadema hawawachukii wawekezaji, lakini wanachohitaji ni wananchi na wawekezaji kila mmoja kufaidi rasilimali za nchi.
Mbowe alisema watu, ambao Chadema ina ugomvi nao ni viongozi waliofungua
 milango na kuruhusu wawekezaji wasiokuwa na uwezo kuja kuwekeza nchini.
Kuhusu Katiba aliitahadharisha Tume ya Mabadiliko ya Katiba na serikali 
akisema kama wanajidanganya kuwa watakuja kuwapandikizia katiba 
wanayoitaka, nchini  “hapatatosha”.
“Kama haitakuwa na maslahi ya Watanzania tunaikataa.  Kuandika katiba ni jambo jepesi, bali kuiridhia,” alisema Mbowe.
Alisema katiba ina maeneo mengi yanayohitaji kurekebishwa na kuonya kuwa
 iwapo watayafanyia maskhara hawataikubali na watakwenda kuwahamasisha 
wananchi ili waungane nao kuikataa.
Mbowe alisema Watanzania hawawezi kuwa na serikali mbili katika mfumo wa
 sasa na kupendekeza kuwa Wazanzibari wapewe uhuru wao, ikiwa ni pamoja 
na kutekeleza matakwa ya kuwapo pia na serikali ya Tanganyika.
Kuhusu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), alisema kama CCM wanafikiri 
Chadema watakubali kuingia kwenye uchaguzi na tume iliyopo, “basi 
wameula wa chuya, hatukubali.”
Alisema kadiri Chadema inavyokua ndivyo maadui nao wanavyozidi kukua, 
huku zikitumika mbinu chafu za kuwagawa viongozi na ‘kuwanunua’ wabunge 
wake.
Hata hivyo, alionya kuwa hawatasita kuwachukulia hatua za kinidhamu watu
 wanaotaka kuwavuruga na kusisitiza kuwa: “Tutakula nao sahani moja.”
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment