SIKU moja baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu
na Majini (Sumatra) kutangaza nauli mpya, wadau mbalimbali wa usafiri
nchini wamepinga hatua hiyo wakisema ingeendana na vipato halisi vya
Watanzania pamoja na huduma bora za vyombo husika.
Kaimu Mkurugenzi wa Sumatra, Ahmad Kilima alitangaza juzi kuwa
ongezeko hilo limetokana na maombi ya wadau wa vyombo vya usafiri
nchini, hivyo wameongeza kiwango kwa wastani wa asilimia 24.46 kwa
daladala badala ya asilimia 149 zilizopendekezwa.
Akizungumza na gazeti hili jana, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama
vya Wafanyakazi nchini (Tucta), Nicolaus Mgaya alisema suala hilo ni
zito na litawaumiza wafanyakazi kwa kuwa litakuwa ni mzigo mkubwa kwao.
Alisema kwa sasa wafanyakazi hawaridhishwi na kima cha chini
wanacholipwa, kwamba maisha yatakuwa juu na hivyo baadhi ya familia
watoto watashindwa kwenda shule kabisa.
“Kupanda kwa nauli kutawaumiza watu wengi na wanafunzi wataumia zaidi,
sidhani kama mzazi atakuwa na uwezo wa kumpa mwanafunzi nauli huku yeye
mwenyewe akiwa anabanwa kwa mshahara mdogo anaolipwa,” alisema Mgaya.
Alidai kuwa serikali inaangalia zaidi mwekezaji kuliko kujali raia
wake huku akitolea mfano wawekezaji wa mafuta na vyombo vya abiria bila
kujali wananchi wanagandamizwa pia.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Bara, Julius Mtatiro
alisema kupandisha nauli, serikali imewabebesha mzigo mkubwa wananchi
tena bila kuangalia huduma ya vyombo vya usafiri.
Alisema kabla ya nauli kupanda serikali na wadau wa vyombo vya usafiri
walitakiwa kuangalia kama huduma zao zimeboreshwa ndipo wapandishe
nauli kulingana na mahitaji bora ya wananchi.
Mtatiro alifafanua kuwa hata kabla ya nauli kupanda watu walikuwa
wanatembea kwa miguu kutokana na kutokuwa na uwezo wa kupanda daladala
kwa sh 300 hadi 500.
“Hata wengine walishindwa kwenda kwao mikoani na hivyo hujichangisha
na kwenda mara moja kila baada ya miaka mitano, sasa watashindwa kabisa
kufanya hivyo,” alisema.
Alisema serikali ina mipango mibovu isiyozingatia maslahi na kipato
kwa wananchi, na kuishauri kuliangalia suala hilo kwa mapana zaidi kabla
ya utekelezaji wake kuanza.
Mmoja wa wananchi, Ruhazi Ruhinda alisema kuwa kiwango hicho
kilichoongezeka kimewekwa kwa nia ya kuwaua wanyonge kwa vile hakiendani
na hali halisi ya kipato cha Mtanzania wa hali ya chini.
“Mwananchi wa kipato cha chini mshahara wenyewe hautoshi, hivyo badala
ya kufikiria kuongeza nauli hizo wangefikiria kuboresha miundombinu na
huduma za usafiri kwanza,” alisema.
Aliongeza kuwa mamlaka husika zimekuwa hazitendi haki kwa wananchi,
kwani awali umeme nao ulipandishwa bila kuzingatia uwezo wa vipato vya
watu.
“Upandishwaji huu umefanywa kiholela, baada ya muda vyakula navyo havitakamatika kwa kisingizio cha nauli,” alisema.
Mwenyekiti wa Chama cha Kutetea Abiria (Chakua), Hassan Mchanjama
alisema wanapinga utaratibu wa Sumatra kupandisha nauli kwa asilimia 40
bila kujali kipato cha watu wa kawaida.
Akizungumza jana na gazeti hili alidai wameshtushwa na kitendo hicho
ambacho kinadhihirisha wazi kuwa sekta nyingi za kijamii nchini
zinashikiliwa na mafisadi wasiojali ugumu wa maisha.
Alisema wanapinga kupanda huko kutokana na utaratibu mbaya wa Sumatra
wa kushindwa kuwasimamia wamiliki wa magari, madereva na makondakta
katika uendeshaji wa huduma hiyo nchini.
Alitaja baadhi ya maeneo ambayo miaka yote yamekuwa yakilipa nauli
tofauti na ile elekezi ya serikali kuwa ni Mbagala, Mbezi na
Gongolamboto.
“Unajua hapa kuna ufisadi kwani katika kikao chetu cha Desemba mwaka
jana, kati yetu, Sumatra na wamiliki wa magari tuliwapinga wasipandishe
nauli hadi pale watakapoleta mchanganuo wao unaotuonesha kuwa wanapataje
hasara katika uendeshaji,” alisema.
Alisema kuwa wamiliki walishindwa kutekeleza makubaliano hayo kitendo
kinachodhihirisha wazi kuwa biashara hiyo inaendeshwa kihuni bila ya
kutunza mahesabu.
No comments:
Post a Comment