MAHAKAMA ya Wilaya  ya Igunga, mkoani Tabora imemhukumu 
kutumikia kifungo cha miezi sita jela  mshitakiwa Lupembe Majebele (25),
 mkazi wa Kijiji cha Lutende, Wilaya ya Uyui  mkoani Tabora kwa kosa la 
kuendesha pikipiki bila leseni.
Awali akisomewa  mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama 
ya Wilaya ya Igunga, Ajali  Milanzi, Mwendesha Mashtaka wa Polisi 
Dezidery Kaigwa aliiambia mahakama kuwa  mshitakiwa anakabiliwa na 
makosa mawili.
Aliiambia mahakama  kuwa kosa la kwanza ni kuendesha chombo cha moto 
bila leseni kinyume na sheria  ya usalama barabarani ya mwaka 1963 
iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002  inayozuia kufanya makosa kama hayo 
na kosa la pili ni kumgonga mtembea kwa  miguu na kusababisha kifo 
chake.
Mwendesha mashitaka  huyo aliendelea kuiambia mahakama kuwa mnamo 
Septemba 10 mwaka huu, majira ya  saa 4:00 asubuhi katika Tarafa ya 
Simbo wilayani hapa, mshitakiwa akiwa  anaendesha pikipiki yenye namba 
za usajili T 200 BZT aina ya Sanlg aliendesha  kwa uzembe na kumgonga 
Kulwa Robert mkazi wa Simbo na kusababisha kifo chake.
Baada ya kusomewa  mashitaka yote mawili, mshitakiwa alikana shitaka 
la kuua na kukiri shitaka la  kuendesha chombo cha moto bila leseni.
  Baada kukiri kosa  hilo moja, mahakama ilimtia hatiani kutumikia 
adhabu ya kifungo cha miezi sita jela  na kesi ya kuua bado inaendelea. 
Itatajwa tena Oktoba 10, mwaka huu.
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment