HATIMAYE msanii wa filamu nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’, jana
 alipata dhamana baada ya kutimiza masharti matano aliyopewa na Mahakama
 Kuu Kanda ya Dar es Salaam, juzi.
  Lulu anakabiliwa na kesi ya kumuua bila kukusudia aliyekuwa msainii mwenzake Steven Kanumba.
Lulu alitimiza masharti hayo jana saa 9 alasiri kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Francis Kabwe.
Baada ya kutimiza masharti hayo ya dhamana, aliwaeleza waandishi wa 
habari huku akitokwa machozi kuwa anamshukuru Mungu, kwani yeye ndiye 
alifanya akapata dhamana hiyo na hivyo kumfanya atoke gerezani na 
kurejea kuishi uraiani.
Lulu ambaye alikuwa ameongozana na wakili wake Peter Kibatara, alisema
 anawashukuru wale wote waliokuwa naye bega kwa bega, tangu kesi yake 
ilipoanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.
“Ninachoweza kusema ni kuwashukuru wale wote waliokuwa wakinihangaikia
 na kuniombea kwa Mungu hadi leo nimepata dhamana, narudi kuungana na 
familia yangu…lakini naomba watu hao waendelee kuniombea, kwani leo 
nimepata dhamana tu na ile kesi yangu ya msingi ya kuua bila kukusudia 
bado haijaanza kusikilizwa na kutolewa uamuzi, hivyo naombeni sana 
waendelee kuniombea na wasinitupe,” alisema Lulu.
  Msanii huyo amedhaminiwa na Florian Matungwa, ambaye anatoka Wizara ya Ardhi na Verus Mboneko Wizara ya Afya.
Lulu alifikishwa eneo la Mahakama Kuu saa 7:58 mchana na gari ya Jeshi
 la Magereza lenye namba za usajili STK 2823. Baada ya kupatiwa dhamana,
 aliondoka na gari aina ya Land Cruiser VX V8, lenye namba za usajili 
T480 CFX.
Hata hivyo, Wakili Kibatara, aliwaeleza waandishi wa habari kuwa kwa 
niaba ya mteja wake, anakanusha uvumi uliokuwa umeenea kuwa Lulu 
angeliachiwa kwa dhamana jana angeenda moja kwa moja kwenye kaburi 
alilozikwa Kanumba lililoko eneo la Kinondoni na kuongeza kwa kumshukuru
 Msajili Kabwe, kwa kumpatia dhamana mteja wake, kwani muda wa kazi 
ulikuwa umepita.
Mawakili wa Lulu, Peter Kibatara, Kennedy Fungamtama na Fulgence 
Massawe waliiomba mahakama hiyo impatie dhamana mshtakiwa huyo ambaye 
amesota rumande katika gereza la Segerea tangu Aprili mwaka jana, ambapo
 walieleza kuwa ombi la dhamana wameliwasilisha chini ya kifungu cha 
  148(1), (2) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai ya mwaka 2002 .
Jaji Mruke alisema ili mahakama impatie dhamana ni lazima asalimishe  
kwa Msajili wa Mahakama hiyo hati ya kusafiria,  kutotoka nje ya Dar es 
Salaam  bila ruhusa ya mahakama, kuripoti kwa msajili kila mwezi, kuwa 
na wadhamini wawili ambao ni watumishi wa serikali  ambao watasaini 
bondi ya sh milioni 20 kila mmoja.
  Baada ya jaji huyo kutangaza masharti hayo, Lulu alishindwa kupata 
dhamana hiyo baada ya Msajili wa Mahakama kutokuwepo ofisini hiyo juzi.
  Wasanii waliokuwepo kumuunga mkono Lulu mbali na mama yake mzazi 
mahakamani hapo, ni Mahsein Awadh maarufu Dk. Cheni, Muna na msanii 
mwingine ambaye jina lake halikupatikana mara moja.
 
 
 
 
 
 
 

 
No comments:
Post a Comment