JESHI la Polisi wilayani Bunda linamshikilia Elifinya Batholomeo
 (28), mkazi wa jiji la Dar es Salaam kwa tuhuma za kumgonga mwanafunzi 
wa darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Kabalimu, Maria Peter (7), na
 kusababisha kifo.
Tukio hilo limetokea juzi saa 10:00 jioni katika eneo la mtaa wa 
Posta, barabara ya Musoma –Mwanza, ambapo mwanafunzi huyo alikuwa 
akitembea kando ya barabara.
  Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo gari hilo lilikuwa katika mwendo
 kasi wakati likipishana na gari jingine ndipo lilipomgonga mwanafunzi 
huyo ambaye alikufa papo hapo.
  Walisema kuwa dereva huyo ambaye alikuwa akiendesha gari aina ya 
Pajero lenye na T 651 
BMZ mali ya kampuni ya Geodata, baada ya kubaini 
kuwa ameua, hakusimama kutokana na kuhofia maisha yake.
  Aidha mashuhuda hao walilazimika kutoa taarifa polisi ambao walifika 
na kuchukuwa mwili wa mwanafunzi huyo ambao umehifadhiwa katika 
hospitali ya wilaya.
  Walisema kuwa baadaye polisi walilifuatilia gari hilo ambalo lilipitia
 njia za mkato na kufanikiwa kulikamata katika kijiji cha Nyamatoke.
Akizungumzia tukio hilo mama wa mwanafunzi huyo aliyejitambulisha kwa 
jina la Ghati Wambaura alisema kuwa mtoto wake aliondoka siku hiyo 
asubuhi kwenda kanisani lakini majirani walimpa taarifa juu ya kugongwa 
na gari.
  “Mtoto wangu huwa anashinda kanisani na wenzake lakini ilipofika jioni
 niliambiwa na watu kuwa kuna mtoto amegongwa na nilipoenda polisi na 
kujulishwa kuwa mwili upo hospitali ndipo nilipobaini kuwa ni mtoto 
wangu,” alisema.
  Polisi walisema kuwa wanatarajia kumfikisha mahakamani dereva huyo ili kujibu tuhuma zinazomkabili.
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment