SERIKALI imetangaza kuwapatia mikopo  wanafunzi wa elimu ya juu 
29,754 kati ya wanafunzi 31,647 katika mwaka wa  masomo 2013/2014.
Mkurugenzi wa Habari, Elimu na  Mawasiliano, Bodi ya Mikopo ya 
Wanafunzi wa Elimu ya Juu, Cosmas Mwaisobwa,  alieleza hayo jijini Dar 
es Salaam jana alipozungumza na waandishi wa habari  kuhusu utaratibu wa
 utoaji wa mikopo hiyo kwa wanafunzi wapya na wanaoendelea na  elimu ya 
juu.
Alisema uchambuzi wa maombi ya mikopo kwa  mwaka huu wa masomo 
umekamilika na kwamba lengo la serikali ni kuwawezesha  wanafunzi wa 
elimu ya juu kupata fedha kwa muda muafaka.
Alisema kuwa mchanganuo wa utuoaji wa  mikopo hiyo ulizingatia vigezo na masharti ya uombaji mikopo na ruzuku.
Alisema idadi ya waombaji wapya  waliotuma maombi yalikuwa 53,239, 
waombaji wanaoendelea na masomo 43,032,  waombaji waliokuwa na maombi 
yenye matatizo ni 6,364.
“Wengine ni waombaji waliorekebisha  matatizo kwenye maombi yao 3,151 
na waombaji ambao hawakurekebisha matatizo  kwenye maombi yao 3,213,” 
alisema.
Akifafanua zaidi kuhusu mchanganuo huo  alisema waombaji wapya 53,630 watakaosoma   ndani na nje ya nchi wamepata mikopo hiyo.
Alisema maombi ya mikopo kwa wanafunzi  wanaoendelea 61,692 ambao 
wanasoma ndani na nje ya nchi wamepangiwa kupata  mikopo hiyo.
Mkurugenzi   huyo alisema bodi ya mikopo ya elimu ya juu inatarajia 
kutoa mikopo ya  sh bilioni 306 kwa ajili ya ukopeshaji wanafunzi wapya 
na wanaoendelea na  masomo.
Alisema mchakato wa upangaji wa mikopo  unaendelea vizuri na kwamba hadi sasa umekamilika kwa zaidi ya asilimia 90.
“Matarajio ni kukamilisha mchakato huu kwa  asilimia 100 ifikapo wiki 
ya kwanza ya Oktoba kabla ya vyuo vya elimu ya juu  kufunguliwa, kwa 
mujibu wa Tume ya Vyuo Vikuu,” alisema.
Alieleza kuwa orodha kamili ya waombaji wapya  waliopangiwa mikopo 
inapatikana kwenye tovuti ya bodi hiyo www.heslb.go.tz  ambapo mwombaji 
anaweza kutafuta jina lake kwa kutumia namba ya mtihani ya  kidato cha 
nne.
Alisisitiza kuwa taratibu za kupeleka  mikopo yao vyuoni zinaendelea na kwamba watalipwa baada ya kufanya usajili.
Aidha alisisitiza umuhimu wa kila  mwombaji kuwa na akaunti ya benki kwa ajili ya kupitishia mikopo hiyo.
  Aliongeza kusema kuwa waombaji waliofanikiwa  kupangiwa mikopo 
wanawajibika kurejesha mikopo hiyo baada ya kuhitimu masomo  yao. 
 
 
 
 
 
 
 

 
No comments:
Post a Comment