Jeshi la Polisi litapeleka askari
wake Afrika Kusini kuwahoji washiriki wa video za wasanii wa muziki wa
Bongo fleva, Agnes Gerald ‘Masogange’ na mwenzake Melisa Edward
waliokamatwa nchini humo na dawa za kulevya.
Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia Dawa za
Kulevya, Godfrey Nzowa aliiambia Mwananchi kwa simu jana kuwa
watawapeleka polisi kuwahoji na wanaamini wahusika watawaeleza wahusika
wa mzigo huo.
Wasichana hao walikamatwa kwenye
Uwanja wa Ndege wa Oliver Tambo nchini Afrika Kusini wakitokea Tanzania
wakiwa na kilo 150 za dawa za kulevya aina ya Crystal Methamphetamine.
“Tutawapeleka askari wetu kuwahoji,
tumekwishaanza uchunguzi wa hili...wote watakaohusika katika hili
tutawakamata, lakini tunakwenda polepole hatua kwa hatua kuhakikisha
tunawanasa wahusika sahihi,” alisema Nzowa.
Naye Mkurugenzi wa Uwanja wa Ndege wa
Julius Nyerere, (JNIA), Moses Malaki alieleza kushangazwa na kiasi
kikubwa kupitishwa kwenye uwanja huo licha ya kuwa wapo watu wenye
dhamana ya kuangalia usalama.
“Sitaki kusema tutafanya nini, lakini
ninachotaka kukwambia ni kwamba uchunguzi umeanza na suala zima
tumewaachia polisi na sisi tutatoa ushirikiano kwa kila hatua
watakayotutaka, lazima kukomesha hili.
“Tutaangalia nani walikuwa zamu siku hiyo,” alisema Malaki
No comments:
Post a Comment