Katika
kuelekea siku ya wanawake duniani,iliyoadhimishwa Duniani kote mnamo
Machi 5, kampeni ya Grow ikiongozana na mmoja wa mabalozi wake muigizaji
Jacob Stephen ‘JB’ iliungana na kipindi cha EATV Nirvana na kuutembelea
mji wa Lushoto,Jijini Tanga.
Kampeni
ya GROW, inayoendeshwa na Oxfam, inahamasisha mabadiliko kwenye mifumo
iliyopo ili iwafanufaishe wakulima na wafugaji/wavuvi wadogo wadogo
hususani wanawake wawe na maisha endelevu! Inawasherekea kwa mchango wao
mkubwa wa kulisha nchi huku wakipambana na changamoto nyingi ikiwemo
ukosefu wa masoko, pembejeo na miundo mbinu. Katika harakati hizi, mnamo
mwaka 2011, shindano la "Mama Shujaa wa Chakula " lilizinduliwa rasmi
hapa nchini. Lengo la tuzo hii ni kutambua mchango wa wanawake hasa
waishio vijijini.
Huko Lushoto hali ilikuwa kama picha zinavyoonyesha...
Alfajiri
ya Machi 6, timu ya Nirvana, Grow, pamoja na JB walielekea soko kuu la
Lushoto ambapo walikutana na wakulima ili kusikia hadithi zao za
mafanikio pamoja na changamoto. Nirvana na Kampeni ya GROW wanahamasisha
lifestyle njema! Lakini tunavyokula vyakula bora, vyenye virutubisho
tunajua vinatoka wapi!
Akizungumza
kutoka katika sehemu yake ya biashara, Zinira Ally (kushoto aliyekaa)
alishuhudia jinsi ambavyo anasomesha watoto na kulisha familia yake kwa
pesa inayotokana na biashara yake ya uuzaji wa mbogamboga na matunda.
"Nzenze"... Salaam na wapenzi wa filamu zikiendelea.
JB, Lotus na Deo wakitizama mazao mbalimbali katika soko kuu la Lushoto.
Veronica
Joseph ambaye ni muuzaji wa mboga mboga sokoni Lushoto anasema
angependa kuona mabadiliko katika miundombinu ya soko ili kulinda ubora
wa mazao, “soko halina ubora, watu wananunua vyakula hivi hivi kwa bei
ghali kwenye supermarket kwa sababu ya ubora, sie tunauza tu bora
tunauza, tunaogopa vyakula kuoza, tungekuwa na mafriji ya kuhifadhia
mboga mboga na sisi tungeweza kuuza bei sawa na supermarket.”Akiendelea
kutaja changamoto, Veronica ambaye ni mama wa watoto wawili, alionyesha
kusikitishwa kwake na maisha duni wanayoishi wakulima, “mkulima analima
chakula ambacho wengine wanakula hadi kutupa lakini yeye hawezi hata
kula mlo kamili kwa sababu kipato anachopata ni kidogo”
Veronica anaamini kama, “masoko yangeboreshwa, tungeuza bidhaa kwa bei
nzuri ili na sisi tusomeshe watoto wetu na kujikimu kimaisha.”