Pemba,16th August, 2012: Kampuni ya simu za mikononi ya Zantel imetoa nguo pamoja na vyakula kwa ajili ya Idi kwa nyumba ya kutunza wazee wasiojiweza ya Limbani pamoja na ile ya waathirika wa ukoma wa Makundeni hapa mkoa wa kaskazini Pemba.
Msaada huo unaojumuisha mafuta ya kupikia,mbuzi,sukari,tambi, tende pamoja na maharage umetolewa leo katika hafla fupi ya makabidhiano kwenye vituo hivyo.
Nyumba hizo ambazo ziko chini ya ustawi wa jamii Zanzibar, ya Limbani ikiwa na wazee wasiojiweza huku kijiji cha Makundeni kikiwa kinatunza waathirika wa ukoma zinasaidia wazee na waathirika wa ukoma kwa kuwapa fedha ya kujikimu pamoja na makazi.
Nyumba ya Limbani ina wazee nane na kijiji cha Makundeni kina wakazi 62, wanaume 34 na wanawake 28.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo kwa wazee wa vijiji hivyo, mkurugenzi wa biashara wa Zantel-Zanzibar, bwana Mohammed Mussa, amesema ni kawaida kwa kampuni ya Zantel kusaidia makundi mbalimbali ya kijamii katika kipindi hiki cha Ramadhani.
'Wazee ni sehemu muhimu sana ya jamii,lakini mara nyingi wanasahaulika sana na ndio maana Zantel tumeamua kuja hapa Pemba leo kutoa msaada huu ambao unatutofautisha sana na makampuni mengine katika vipaumbele vyetu' alisema Mussa.
Naye mkuu wa idara ya ustawi wa jamii Pemba, Abduu Salim Mohammed aliwashukuru Zantel kwa msaada huo, akisema umekuja kwa wakati mufaka hasa ukizingatia kuwa wanakaribia kuadhimisha sikukuu ya Idi.
'Kwa misaada hii, Zantel inawafanya wazee nao wajiskie sehemu ya jamii, kwani mara nyingi wamekuwa wakisahaulika sana' alisema Maalim Abduu.
Kampuni ya Zantel imekuwa msitari wa mbele katika kusaidia makundi mbalimbali ya kijamii kipindi hiki cha mwezi wa Ramadhani, na msaada huu ni maalumu kwa kundi la wazee ambalo mara nyingi linasahaulika katika jamii.
No comments:
Post a Comment