MEYA wa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba, Dk. Anatory Amani
(CCM) amejiweka katika wakati mgumu wa kung’olewa wiki ijayo baada ya
kukimbia kikao cha madiwani wa chama hicho kilichokuwa kimjadili.
Katika kikao hicho kilichotawaliwa na vurugu za kurushiana viti baina
ya pande zinazopingana, Amani alitumia janja ya kuumwa na hivyo
akaondoka kikaoni baada ya katibu wa kikao hicho na msaidizi wake nao
kuondoka kwa staili hiyo.
Meya Amani anatuhumiwa na baadhi ya madiwani wa manispaa hiyo kuwa,
ametumia vibaya madaraka yake, akijihusisha na vitendo vya ubadhirifu,
na hivyo kikao hicho cha madiwani wa CCM kilikuwa kijadili na kupata
muafaka wa ama ang’oke mwenyewe au asubiri kupigiwa kura Januari 22.
Tayari madiwani nane wa chama hicho akiwemo Mbunge wa Bukoba Mjini,
Balozi Khamis Kagasheki na wengine wawili wa upinzani wametia saini hati
ya kumtaka mkurugenzi wa halmashauri hiyo, aitishe kikao cha dharura
ili kumng’oa meya huyo.
Habari za ndani kutoka kwenye kikao hicho cha kamati ya uongozi wa
madiwani, zilisema kuwa mvutano ulianza mapema kwa wajumbe kupinga Amani
asiongoze kikao hicho kwa vile ni mtuhumiwa.
Hata hivyo, vuta ni kuvute hiyo iliendelea na hivyo Amani akaongoza
kikao hicho, lakini akalalamikiwa kwa kuwapendelea wale wanaomuunga
mkono hatua iliyomkasirisha Diwani wa Kata ya Nyanga, Deusidedit
Mutakyahwa kunyanyua kiti na kumpiga Diwani wa Kata ya Kahoro, Chief
Karumuna, aliyekuwa akichangia na kumtetea meya huyo.
“Baada ya vurugu hizo Amani alimshawishi Mutakyahwa aende polisi,
lakini wajumbe wakawasuluhisha kwa madai kuwa ni ugomvi wa makundi yao.
Na kikao kilipoonekana kumbana meya, ghafla katibu aliomba udhuru wa
kuondoka,” alisema mtoa taarifa.
Katibu huyo ambaye ni diwani wa viti maalum, Ashura Hassan alidai
mtoto wake anaumwa na hivyo kukasimu madaraka yake kwa msaidizi wake,
Diwani wa Kata ya Nshambya, Hilde Blandus, ambaye pia baada ya kupokea
kiti aliomba udhuru akidai mama yake ni mgonjwa.
“Huu ulikuwa ni ujanja
uliopangwa mapema kwani hata Meya Amani muda mfupi alidai kuwa amechoka
kutokana na sindano za Quinine hivyo asingeweza kuendelea na kikao,
akaondoka bila kukifunga,” alisema.
Kwamba Amani aligoma pia kuwapa wajumbe muhtasari wa kikao cha kamati
ya siasa ya wilaya kilichopita akidai kuwa katibu aliondoka nao.
Kufuatia hali hiyo, madiwani waliazimia kusonga mbele na hoja yao
katika kikao cha ‘full council’ cha wiki ijayo Januari 22, kitakachoamua
kwa kura za madiwani wa vyama vyote kama ang’oke au la.
Taarifa za ndani zinadai kuwa, rushwa imeanza kutembezwa kwa baadhi ya
madiwani wa vyama vyote ili kuwarubuni wasipige kura ya kumng’oa meya.
Baadhi ya vigogo wa serikali akiwemo mkuu wa wilaya na mkoa,
mwenyekiti na katibu wa chama tawala Mkoa wa Kagera, wamekuwa wakifanya
kila juhudi kumnusuru Amani asing’olewe.
Halmashauri hiyo ina madiwani 24; watatu wa CUF, wanne wa CHADEMA na
17 wa CCM. Ili kupitisha uamuzi huo wa kumuondoa meya, ni lazima robo
tatu ya madiwani, yaani 16, wapige kura ya kuunga mkono hoja hiyo.
Miongoni mwa vigogo waliosaini hati ya kutaka kuitishwa kikao cha
kumng’oa meya huyo ni Naibu wake, Alexander Ngalinda (Diwani wa Kata ya
Buhende) na Yusuf Ngaiza (Kashai) ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM
Manispaa ya Bukoba.
No comments:
Post a Comment