SAKATA la uwanja wa wazi wa kidongo chekundu kubadilishwa
matumizi lachukua sura mpya baada ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya
Dar es Salaam na Shule ya Msingi Gerezani kupanga kuandamana ili
kushinikiza kurudishiwa kiwanja hicho.
Miezi michache manispaa ya Ilala walioutupia lawama uongozi wa manispaa hiyo kwa
kukigeuza kiwanja cha Kidongo Chekundu kuwa eneo la kuuzia magari.
Wakizungumza baadhi ya wanafunzi
wanaosoma katika shule hizo zilizoko jirani na kiwanja hicho, walidai
kushangazwa na hatua iliyofikiwa na uongozi wa manispaa hiyo kuamua
kukifanya kiwanja hicho kuwa sehemu ya kuuzia magari chakavu.
Mwanafunzi aliyejitambulisha kwa jina moja la Mussa, alisema kuwa
wamechoshwa na ufisadi unaofanyika katika manispaa hiyo hivyo
wanalazimika kuandaa maandamano yatakayoelekea katika ofisi ya mkuu wa
mkoa ili kushinikiza kuondolewa kwa magari hayo.
Alisema kuwa kutokana na kukosa eneo la kufanyia mazoezi na huku
baadhi ya wanafunzi wasichana wakidai kupata vishawishi vya kimapenzi
kutoka kwa watu wanaokaa katika eneo hilo ni muhimu suala hilo likapata
utatuzi.
“Tunataka kujua wanakusanya kiasi gani maana kama faida ipo ni muhimu
ikagawanywa kwa shule zilizopo jirani kuliko faida kutumiwa na watu
wachache ambao wamegeuza eneo hilo kuwa mradi wao,” alisema.
Naye Asha Aidy, alisema kuwa sasa hivi wanaogopa hata kupita eneo hilo
kutokana na kuwepo kwa vitendo vya vishawishi vinavyotoka kwa watu
wanaouza magari hayo.
Alisema kuwa manispaa hiyo ina maeneo mengi ya kuweka maduka ya
magari chakavu na sio kukitumia kiwanja hicho ambacho ni mahususi kwa
shughuli nyingi za kijamii.
Hata hivyo, gazeti hili lilijaribu kumtafuta diwani wa eneo hilo,
Salum Bisarara (CCM), ili kupata kauli yake, ambapo alikiri kuwepo kwa
maegesho ya magari lakini alitaka kuiuliza manispaa ndiyo yenye kujua
ukweli.
Akizungumza kuhusu malalamiko hayo, ofisa mahusiano wa manispaa hiyo,
Tabu Shaibu, alisema kuwa hana taarifa za kuwepo kwa maandamano hayo
lakini alikiri uamuzi wa kuweka maegesho wa magari ulifikiwa na manispaa
hiyo.
Alisema kuwa manispaa ilianza kukusanya mapato tangu Desemba mwaka jana kupitia maegesho hayo.
No comments:
Post a Comment