MBIO za kuchukua na kurejesha fomu za kuwania nafasi mbalimbali
katika Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), zilizoanza Januari 14,
zimefungwa jana saa 10:00 jioni, huku wadau 45 wakijitokeza.
Uchaguzi huo utafanyika Februari 24, baada ya uongozi wa sasa chini ya rais wake Leodegar Tenga kumaliza muda wake.
Idadi hiyo ni jumla ya wadau waliojitosa kwenye nafasi zote nne,
ambazo ni rais, makamu wa rais na ujumbe wa kamati ya utendaji ambao
wameomba kupitia kanda zao.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, wagombea 11
wamejitokeza siku ya mwisho ambao walichukua fomu na kuzirejesha jana
hiyo hiyo.
Aliyechukua fomu jana kwa nafasi ya Mwenyekiti ni Richard Rukambura,
ambaye atachuana na Jamal Malinzi, Athuman Nyamlani na Omari Nkwarulo
katika vita ya kurithi kiti cha Tenga.
Walioongezeka jana kwa nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni
Kaliro Samson, Jumbe Magati, Richard Rukambura, Omari Walii, Ahmed
Mgoyi, John Kiteve, Stanley Lugenge, Francis Ndulane, Riziki Majala na
Hassan Othuman Hassanoo.
Mbali ya waliofika kwenye ofisi za TFF kuchukua na kurejesha fomu
hizo, kwa wagombea wa mikoani waliweza kutumia tovuti ya shirikisho hilo
na kurejesha kwa barua pepe.
Orodha kamili ya wagombea ni Malinzi, Nyamlani, Nkwarulo na Rukambura
kwa nafasi ya rais huku makamu wa rais ikiwa na wagombea watatu, Michael
Wambura, Ramadhan Nassib na Wallace Karia.
Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ni Salum Chama na Kaliro Samson (Kagera
na Geita), Jumbe Magati, Mugisha Galibona, Richard Rukambura, Samuel
Nyalla, Titus Osoro na Vedastus Lufano (Mara na Mwanza).
Wengine ni Epaphra Swai na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu),
Charles Mugodo, Elly Mbise na Omari Walii (Arusha na Manyara), Ahmed
Mgoyi na Yusuph Kitumbo (Kigoma na Tabora), Ayubu Nyaulingo, Blassy
Kiondo, Nazarius Kilungeja na Selemani Kameya (Katavi na Rukwa), na
James Mhagama na Stanley Lugenge (Njombe na Ruvuma).
Wadau wengine ni Athuman Kambi, Francis Ndulane na Zafarani Damoder
(Lindi na Mtwara), Hussein Mwamba na Stewart Masima (Dodoma na Singida),
Farid Nahdi, Geofrey Nyange, Hassan Othman Hassanoo, Riziki Majara na
Twahili Njoki (Morogoro na Pwani).
Wengine ni Elias Mwanjala, Eliud Mvella na John Kiteve (Iringa na
Mbeya), Khalid Mohamed (Kilimanjaro na Tanga) na Muhsin Balhabou, Omari
Abdulkadir na Shaffih Dauda (Dar es Salaam).
Kwa upande wa Bodi ya Ligi Kuu, wagombea watano wamejitokeza kuwania
nafasi mbalimbali katika chombo hicho hadi zoezi la uchukuaji na
urejeshaji wa fomu linafungwa.
Mbali ya Yusuf Manji wa Yanga aliyeomba uenyekiti, pia yupo Ahmda
Yahya wa Kagera Sugar, Saidi Mohamed wa Azam aliyejitosa kwenye umakamu
huku Christopher Peter wa Moro United na Kazimoto Miraji wa Pamba ya
Mwanza wameomba ujumbe wa bodi kuwakilisha klabu za Ligi Daraja la
Kwanza.
No comments:
Post a Comment