JOTO la kupunguziwa madaraka ya uteuzi kwa rais, limezidi
kupanda ambapo sasa Tume ya Uchaguzi (NEC) nayo imependekeza iondolewe
chini ya rais, badala yake iwe chini ya Bunge.
Tume hiyo, imesema imefikia uamuzi huo baada ya kutafakari madai ya
wadau wengi ambao wamekuwa wakishutumu utendaji wake, kwamba umelenga
kukipendelea Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika maamuzi yake.
Imetaka wajumbe wake wasiteuliwe na rais kama ilivyo sasa, badala yake
majina yao yapendekezwe na jopo maalumu, kisha yathibitishwe na Bunge
kabla ya kupelekwa kwa rais.
Kutokana na mapendekezo hayo, sasa kazi ya rais itakuwa kuteua majina
ya wajumbe wa tume hiyo. Kadhalika, tume inataka rais asiwe na mamlaka
ya kuwafukuza kazi wajumbe wake, bali jukumu hilo libaki mikononi mwa
jopo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana,
Mwenyekiti wa Tume hiyo,
Jaji mstaafu Damian Lubuva, alisema pia
wanataka wajumbe wa tume waapishwe na jaji mkuu ili kuondoa wasiwasi wa
kuwa watii kwa rais ambaye pia anakuwa mwenyekiti wa chama
kinachotawala.
Katika maoni yao kwa ajili ya katiba mpya, Jaji Lubuva alisema
wanataka pia wajumbe wa tume wasiteuliwe kwa kuzingatia kiwango cha
elimu, bali wazingatie sifa nyingine zikiwemo za uadilifu, heshima,
uwajibikaji na namna anavyokubalika katika jamii ya Watanzania.
Kufukuzwa kwa kiongozi
Katika mapendekezo yake, Tume ya Uchaguzi pia imetaka kufanyika kwa
mabadiliko yatakayowawezesha viongozi wa kisiasa wanaohama, ama
kufukuzwa na vyama vyao kubaki katika madaraka hadi mwisho wa muda wao
wa uongozi.
Jaji Lubuva alisema iwapo mbunge au diwani atafukuzwa au kuhamia chama
kingine, basi ahame na kiti chake cha uwakilishi ili kuzuia matumizi
makubwa ya gharama za kufanya uchaguzi mdogo.
Kwa mujibu wa utaratibu wa sasa, kiongozi wa kuchaguliwa anapofukuzwa
ama kuhama chama chake, hulazimika kuachia ngazi, hivyo kuwepo kwa
uchaguzi mdogo kujaza nafasi iliyoachwa wazi.
Katika mapendekezo mengine, tume inataka kuwepo na utaratibu wa wapiga
kura kuwaondoa madarakani wabunge na madiwani ambao hawatawajibika
katika nafasi zao, badala ya mfumo wa sasa unaoruhu kuondolewa kwa
viongozi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji pekee.
Mahakama ya Uchaguzi
Mapendekezo mengine ya tume hiyo ni kuwepo kwa Mahakama ya Uchaguzi
itakayowezesha wadau na wananchi wasiokubaliana na uamuzi wa tume kukata
rufaa kabla ya kuwasilishwa kwa kesi za uchaguzi mahakamani.
Alisema kuwa mahakama hiyo itafanya kazi pale itakapohitajika, na muda
wa kutekeleza majukumu yake uwe wa haraka kutokana na kazi za uchaguzi
zilivyo.
No comments:
Post a Comment