MKAZI wa Nyakato, Amiri Bakari (18) amehukumiwa na Mahakama ya
Hakimu Mkazi Mkoa wa Mara, kutumikia kifungo cha miaka 30 jela, baada
ya kupatikana na hatia ya kumbaka binti mwenye umri wa miaka 16.
Hukumu hiyo ilitolewa juzi mbele ya Hakimu Mkazi, Janeth Msaroche,
baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka.
Awali ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Jonas
Kaijage, kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo Januari 10, mwaka jana,
majira ya saa 3:00 asubuhi katika eneo la Vailet Baa, Mtaa wa Nyakato
mjini Musoma.
Kaijage aliiambia mahakama hiyo kuwa mshitakiwa huyo alimbaka binti
huyo alipopita katika eneo hilo na kumvutia ndani ya nyumba
isiyomalizika kujengwa.
Alidai kuwa mtuhumiwa huyo baada ya kutimiza hatua hiyo alimbaka binti
huyo huku akimtishia kwa panga alilokuwa nalo na kwamba iwapo atapiga
kelele atamuua.
Alisema kuwa mshitakiwa huyo baada ya kufanya unyama huo alitokomea
kusikojulikana huku binti huyo alikwenda kutoa taarifa kwa wazazi wake
waliokwenda katika eneo la tukio na kukuta chupi ya binti huyo, kisha
kutoa taarifa polisi ndipo mshitakiwa alipokamatwa.
Akijitetea kabla ya hukumu, mshitakiwa aliiomba mahakama impunguzie
adhabu huku Hakimu Msaroche akidai kuwa ametoa adhabu hiyo ili iwe
fundisho kwa mshitakiwa na kwa watu wenye tabia kama hiyo.
No comments:
Post a Comment