MKURUGENZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Ilala, Gabriel Fuime,
anadaiwa kusimamishwa kazi kwa tuhuma za ubadhiRifu wa fedha za umma.
Vyanzo vyetu vya habari kutoka ndani ya ofisi hiyo vimedai kuwa
mkurugezi huyo hajaonekana kazini kwa takriban mwezi mmoja sasa.
Ianadaiwa kwamba Fuime anatuhumiwa kujipatia fedha kinyume cha sheria,
fedha ambazo zinatokana na malipo ya mishahara ya askari mgambo.
Inadaiwa kwamba hali hiyo imetokana na mvutano wa muda mrefu kati ya
mkurugenzi huyo na askari mgambo ambao walikuwa wakidai haki zao kama
waajiriwa huku wakilipwa kama vibarua.
Ofisa Habari wa Wilaya hiyo, Tabu Shaibu, alisema hana uwezo wa
kulitolea maelezo jambo hilo kwa kuwa kwa sasa linashughulikiwa na ngazi
za juu.
“Mimi si mtoa taarifa, kwa sababu kama ujuavyo wakurugenzi huteuliwa
na wizara kwa hiyo nenda wizarani watakwambia mimi siwezi kulizungumzia
hilo,” alisema.
Hata hivyo, Fuime alikana kusimamishwa kazi kwa tuhuma hizo, lakini akakiri kwamba kwa sasa ameambiwa apumzike kwa muda.
“Siwezi kukuambia tatizo ni nini kutokana na mazingira yaliyopo, kwa
kuwa tatizo hilo liko kwa wakubwa wangu, hivyo nikilizungumzia kwa
undani nitakuwa nakwenda kinyume cha taratibu za kazi,” alisema.
Hata hivyo, waandishi walipotaka kujua kama alisimamishwa kazi kutokana na hujuma, Fuime alisema hajui chochote kuhusu hilo.
Aliongeza kuwa anachojua ni kuwa kuna mtu ameandika barua ya
malalamiko kuhusu yeye, kwenda Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa (Tamisemi), ambapo hajaisoma hivyo hajui inahusiana na
madai gani.
No comments:
Post a Comment