Mjadala kuhusu masuala ya Muungano unatarajiwa kurejea upya katika kamati za Bunge Maalumu leo, wakati zitakapoanza kujadili sura za saba, nane, kumi na moja, 18 na 15 za Rasimu ya Katiba.
Kamati zimepewa siku sita kujadili sura hizo tano
ambazo zina jumla ya ibara 79, huku miongoni mwake zikigusa masuala
mengi ambayo msingi wake umejengwa juu ya mfumo wa serikali tatu.
Miongoni mwa masuala hayo ni pamoja na baraza la
mawaziri, tume ya kusimamia na kuratibu uhusiano baina ya Serikali ya
Muungano na Serikali za Nchi Washirika (Tanganyika na Zanzibar),
Sekretarieti ya Tume ya Uhusiano na Uratibu, Masuala yanayohusu Benki
Kuu na Fedha pamoja na uteuzi wa watumishi katika Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Suala la aina ya muungano lilianza kujadiliwa katika sura ya kwanza na ya sita katika awamu ya kwanza ya Bunge iliyomalizika mwishoni mwa Aprili mwaka huu na kuzua mvutano mkali ambao hatimaye ulisababisha baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu kususia mchakato huo.
Wajumbe hao ni wale wanaotokana na vyama vya siasa
vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ambao wanataka
mapendekezo yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba ya kuwapo kwa muundo wa
serikali tatu yabaki kama yalivyo na upande mwingine unaowajumuisha
wabunge wengi wa CCM ukitaka muundo wa sasa wa Serikali mbili uendelee.
Kutokana na mvutano huo, Bunge Maalumu
liliahirisha upigaji kura kuamua aina ya muundo unaofaa, lakini hata
liliporejea Agosti 5, mwaka huu halikuweza kupiga kura, badala yake
lilibadilisha kanuni ili kuwezesha upigaji kura kufanyika baada ya
kumaliza mjadala wa sura zote ndani ya kamati.
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad
alisema hakuna maelekezo yoyote yaliyotolewa kwa wajumbe kuhusu jinsi ya
kujadili masuala yanayohusu muungano na kwamba wajumbe watazingatia
mapendekezo waliyoyatoa katika rasimu ya kwanza na ya sita.
“Sidhani kama ni wajibu wetu kutoa maelekezo yoyote, kinachoweza kutokea ni wajumbe kuzingatia kila walichokijadili na kukubaliana katika sura zile za awali, kama walikubali serikali ya shirikisho watazingatia hilo, kama walikubaliana serikali mbili watazingatia hilo pia,” alisema Hamad.
Itakumbukwa kwamba idadi kubwa ya kamati baada ya kujadili sura ya kwanza na ya sita zinazohusu aina ya muungano, zilipendekeza kuachana na muundo wa shirikisho na kuwasilisha maoni yanayotaka kuendelea kwa mfumo wa Serikali mbili. Kamati nyingi zilipata idadi ya kura za kutosha kuunga mkono mapendekezo hayo na chache zilikosa theluthi mbili kutoka kwa wajumbe wa Tanzania Bara na Zanzibar.
Ikiwa kamati hizo zitazingatia uamuzi wake wa awali, basi masuala yote yanayogusa serikali tatu yatafutwa, hivyo zitakuwa na kazi kubwa ya kuandika upya ibara nyingi zinazozingatia utekelezaji wa mfumo serikali mbili.
Maudhui ya Ibara
Ibara ya 98 ya Rasimu pamoja na mambo mengine,
inazungumzia idadi ya mawaziri ambao idadi yao hawapaswi kuzidi 15, huku
uteuzi wao ukipendekezwa uthibitishwe na Bunge.
Ibara ya 99 inazungumzia uwepo wa Waziri Mwandamizi wa Serikali
ya Jamhuri ya Muungano atakayeteuliwa na Rais na kuthibitishwa na Bunge,
wakati Ibara ya 100 (1) inasomeka kuwa: “Waziri Mwandamizi atakuwa na
madaraka ya udhibiti na usimamizi wa utekelezaji wa shughuli za serikali
za siku hadi siku.” Katika sura ya nane inayozungumzia uhusiano na
uratibu wa serikali, Rasimu inapendekeza kuanzishwa kwa tume ya
kusimamia na kuratibu uhusiano baina ya Serikali ya Muungano na Serikali
za Nchi washirika.
Tume hiyo iliyopewa jina la “Tume ya Uhusiano na
Uratibu wa Serikali”, wajumbe wake ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano ambaye atakuwa Mwenyekiti, Rais wa Tanganyika, Rais wa
Zanzibar, Mawaziri Wakazi wanaoziwakilisha nchi washirika katika
Serikali ya Muungano na waziri mwenye dhamana ya mambo ya nje wa
Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
Ibara ya 110 inabainisha kazi za tume hiyo,
utaratibu bora na endelevu wa kushauriana na kushirikiana baina ya
Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali za Nchi Washirika pamoja na
kukuza na kuwezesha uratibu na ushirikiano miongoni mwa nchi washirika
kuhusu mambo yasiyo ya Muungano. Ibara ya 229 inazungumzia masuala ya
fedha na jinsi nchi washirika wa muungano zinavyoweza kukopa fedha
kutoka ndani na nje ya nchi wakati Ibara ya 234 inapendekeza Serikali za
Nchi Washirika kuwa na Benki zitakazokuwa na jukumu la kutunza akaunti
ya fedha za serikali ya nchi mshirika husika na kusimamia sera za
kifedha.
Ibara ya 237 iliyopo katika Sura ya 15
inazungumzia uwapo wa Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa litakalokuwa
na wajumbe kadhaa wakiwamo Makamu wa Rais, Rais wa Tanganyika, Rais wa
Zanzibar na Waziri mwenye dhamana ya ulinzi.
Akizungumzia sura hiyo mtaalamu wa sayansi ya
siasa na utawala katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Alexander
Makulilo alisema Watanzania wasitarajie miujiza katika mijadala
inayogusia muundo wa Serikali.
“Wakati wakijadili sura ya kwanza na ya sita
zilizokuwa zikigusia masuala ya muungano wajumbe walikubaliana juu ya
muundo wa serikali mbili, licha ya kuwa hawakupiga kura ya pamoja kuamua
jambo hilo,” alisema na kuongeza:
“Kwa hiyo katika sura hii ya nane, mtizamo wao
utakuwa uleule kama ilivyokuwa sura mbili zilizopita. Hakutakuwa na
mvutano mkubwa kwa sababu awali walishakubaliana kuhusu muundo wa
serikali mbili. Watanzania wategemee hivyo.”
Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata)
ambalo limeweka kambi Dodoma kushinikiza Bunge hilo kusitishwa, Deus
Kibamba alisema Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilishatoa mwelekeo wa
kuijadili rasimu hiyo lakini haufuatwi.
“Tume ilisema sura ya sita, nane, 10 na 12
zinazungumzia muundo wa Serikali na zijadiliwe kwa pamoja ili upatikane
mwafaka, ushauri ambao haukufuatwa. Kesho (leo) mvutano utakuwa mkubwa
kutokana na hali halisi iliyopo juu ya muundo wa serikali,” alisema.
*Maelezo ya nyongeza na Fidelis Butahe
CHANZO NI GAZETI LA MWANANCHI
CHANZO NI GAZETI LA MWANANCHI
No comments:
Post a Comment